Loading...

Askofu azungumzia matumizi ya chumvi, maji na mafuta katika maombi


ASKOFU wa Kanisa la Morovian Jimbo la Magharibi, Ezekiel Yona, amewataka wachungaji na mashemasi wa kanisa hilo kutojihusisha na vitendo vya udanganyifu vinavyofanywa na baadhi ya wana maombi ambao wamekuwa wakitumia chumvi, maji na mafuta kuwahadaa waumini.

Kauli hiyo aliitoa juzi wakati wa hafla maalumu ya kuliweka wakifu wa jengo jipya la kanisa la Morovian Jimbo la Kahama Mjini pamoja na kuwasimika mashemasi na makasisi 17.

Alisema wako baadhi ya viongozi wa dini wamekuwa wakiwadanganya waumini kutumia chumvi, maji, mafuta na kubusu kinywa cha nguruwe wanapofanyiwa maombi kwamba anaponunua na kuvitumia, anaweza kupona matatizo yake jambo ambalo si kweli.

"Baadhi ya watoa huduma za maombi kwenye madhehebu mengine wanaowanywesha mafuta waumini wao na kisha wanaanguka chini kwa kugalagala na baadaye wanawaombea na kuamka. Vitendo hivi msivifanye na havikubaliki katika kanisa la Mungu," alisema.

Askofu Yona aliwataka makasisi kuendelea kuliombea taifa ili amani iendelee kudumu na kumwombea Rais John Magufuli ili aendelee kuwatetea wanyonge sambamba na kurudisha nidhamu serikalini kwa kusimamia rasilimali za nchi.

Mmoja wa makasisi wapya waliopewa daraja hilo, Emmanuel Sangosango kutoka Kanisa la Morovian kituo cha Mwanza, alisema atahakikisha anakuwa mwaminifu kwa waumini wake na kujiepusha na maombi ya kutumia mafuta na maji.

Naye Yona Mbogo kutoka Singida, alisema atahakikisha anawaelekeza watoa maombi ambao wana tabia ya kuwadanganya waumini juu ya vitu hivyo na kubusu kichwa cha nguruwe ili wapone maradhi, huku wengine wakigeuza maombi kama biashara.

Chanzo: Nipashe
Askofu azungumzia matumizi ya chumvi, maji na mafuta katika maombi Askofu azungumzia matumizi ya chumvi, maji na mafuta katika maombi Reviewed by Zero Degree on 10/22/2019 09:35:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.