Loading...

Uchaguzi wa Rais Nigeria waahirishwa kwa wiki moja

Maafisa wa tume ya uchaguzi wamesema hitilafu za kimipango zimefanya kuwa vigumu kuendelea na uchaguzi

Uchaguzi wa urais na ubunge nchini Nigeria umesukumwa mbele kwa muda wa wiki moja.

Tume huru ya kitaifa ya uchaguzi (INEC) ilitangaza hatua hiyo saa tano tu kabla ya wapiga kura kuelekea katika vituo vya upigaji kura hii leo Jumamosi.

"Haiwezekani kuendelea na zoezi la uchaguzi kama ilivyopangwa," mwenyekiti wa tume hiyo Mahmood Yakubu amesema, akitaja hitilafu za kimipango.

Amesema uamuzi huo mgumu umehitajika kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa huru na haki.

Uchaguzi wa urais na ubunge umepangiwa sasa kufanyika Jumamosi ijayo Februari 23.

Uchaguzi wa Ugavana, wawakilishi wa majimbo na mabaraza ya manispaa yamepangiwa kufanyika Jumamosi Machi 9.

Uamuzi huo umetolewa baada ya mkutano wa dharura katika makao makuu ya tume hiyo ya uchaguzi katika mji mkuu Abuja.


Atiku Abubakar (kulia) na Rais Buhari ni wagombea wakuu miongoni mwa wengine 73 katika uchaguzi wa Nigeria

Ni kwanini Uchaguzi umeahirishwa?

Bwana Yakubu amesema uamuzi huo umechukuliwa baada ya 'ukaguzi wa makini' wa 'mpango ya namna uchaguzi utakavyofanyika', akiongeza kwamba kuna 'jitihada kubwa za kuhakikisha kuna uchaguzi wa huru, haki na wa kuaminika'.

Amesema ni muhimu kuchelewesha uchaguzi huo kuipa tume nafasi ya kukabiliana na masuala muhimu na pia "kusalia na hadhi katika uchaguzi", lakini hakutoa ufafanuzi zaidi.

Katika wiki mbili zilizopita ofisi kadhaa za tume hiyo ya uchaguzi ziliteketezwa moto, huku maelfu ya vifaa vya kunakili kadi , na kadi za upigaji kura zikiharibiwa.

Pia kumekuwa na taarifa ya uhaba wa vifaa vya upigaji kura katika baadhi ya majimbo 36 ya nchi hiyo.

Nigeria imelazimika kushinikiza usalama wake kuelekea katika uchaguzi huu uliokumbwa na ghasia.

Siku ya Ijumaa, maafisa katika jimbo la kaskazini magharibi mwa Nigeria wamearifu kugundua miili ya watu 66, 22 kati yao ni ya watoto, na 12 ya wanawake waliouawa na 'wahalifu'.

Uchaguzi huu ni muhimu kiasi gani?

Mustakabali wa taifa lenye idadi kubwa ya watu barani Afrika na lenye uchumi mkubwa, umo katika mizani.

Yoyote atakayeshinda inabidi ashughulikie masuala kama uhaba wa umeme, rushwa, ukosefu wa usalama na uchumi unaojivuta.

Kuna wagombea 73 waliosajiliwa katika uchaguzi wa urais, lakini kampeni zimegubikwa na Rais Muhammadu Buhari, mwenye umri wa miaka 76, na mpinzani wake mkuu, aliyekuwa makamu wa rais Atiku Abubakar, mwenye umri wa miaka 72.

Buhari anasema amejenga msingi madhubuti kwa ustawi, lakini mpinzani wake anasema Nigeria mambo hayaendi sawa.

Wote wanatoka eneo la kaskazini mwa nchi lenye idadi kubwa ya waislamu. Wakati wote wana umri wa miaka 70, zaidi ya nusu ya idadi jumla ya watu Nigeria, milioni 84 waliosajiliwa kupiga kura wana umri wa chini ya miaka 35.

Je Nigeria imewahi kuwa na matatizo katika uchaguzi?

Ndio. Sio mara ya kwanza uchaguzi umeahirishwa Nigeria - uchaguzi wa awali mnamo 2011 na 2015 ulicheleweshwa kwa siku kadhaa.

Mnamo 2015, taifa hilo liliagiza kufungwa kwa mipaka yake ya nchi kavu na majini kufuatia kuwadia uchaguzi uliokuwa na ushindani mkubwa, huku kukiwepo taarifa kwamba watu wa nchi za nje wanapanga kuingia Nigeria kupiga kura.

Mwaka huo huo, mojawapo ya wagombea alifariki wakati kura zinahesabiwa.
Uchaguzi wa Rais Nigeria waahirishwa kwa wiki moja Uchaguzi wa Rais Nigeria waahirishwa kwa wiki moja Reviewed by Zero Degree on 2/16/2019 08:35:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.