Loading...

Yanga, Azam majaribuni tena leo.

MICHEZO sita ya Ligi Kuu Tanzania Bara inatarajiwa kuunguruma leo katika viwanja tofauti nchini.


Yanga itakuwa kwenye Uwanja wa Kaitaba dhidi ya Kagera Sugar, Azam FC itakuwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi ikiwakaribisha maafande wa JKT Ruvu. Yanga inasaka nafasi ya kuwa karibu na vinara wa ligi Simba inayoongoza kileleni kwa pointi 26. Kwa vyovyote vile, ni lazima ipambane kama kweli inahitaji kuwa karibu.

Timu hiyo inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo ikiwa na pointi 18 nyuma ya Stand United yenye pointi 20 na Simba 26. Tofauti yake na anayeongoza ni pointi nane. Yanga tayari imeshacheza michezo tisa, imeshinda mitano, sare tatu, na kupoteza mmoja. Mabingwa hao watetezi iwapo watashinda mchezo huo watafikisha pointi 21.

Ikiwa wataruhusu kufungwa basi watakuwa kwenye uwezekano wa kushuka katika nafasi ya tatu, kwani walioko nyuma yake wakishinda watapanda juu. Kagera Sugar sio timu ya kubeza, kwani chini ya Kocha Mecky Maxime imekuwa ikijitahidi kufanya vyema.

Huenda ukawa mchezo mgumu kwa kuwa kila mmoja atakuwa anahitaji matokeo mazuri, Kagera ikitaka kushinda kuendelea kubaki nne bora, na Yanga ikitaka ushindi ili kusudi kuwa karibu na wapinzani. Kagera Sugar imeshacheza michezo 11, ikishinda mitano, ikipata sare tatu na kupoteza mitatu ikishika nafasi ya nne kwa pointi 18 sawa na Yanga.

Mchezo mwingine ni Azam FC dhidi ya JKT Ruvu. Timu hii imeshacheza michezo 10, imeshinda mitatu, imepata sare nne, imepoteza mitatu hivyo, ina pointi 13 ikishika nafasi ya nane. Timu hiyo imekuwa haina mwenendo mzuri tangu kuanza kwa Ligi Kuu Tanzania bara. Inacheza na JKT Ruvu ambayo iko hatarini kushuka daraja kwani pia, haiko vizuri.

JKT Ruvu imeshacheza michezo 10, imeshinda mmoja, imepata sare sita, imepoteza mitatu na kufikisha pointi tisa. Hautakuwa mchezo mrahisi kwa kila mmoja, kwa vile wote huhitaji matokeo mazuri kuwa sehemu nzuri. Mtibwa Sugar itawakaribisha Stand United kwenye uwanja wa Manungu, mkoani Morogoro.

Mtibwa Sugar imecheza michezo 11, imeshinda minne, sare nne, imepoteza mitatu na kufikisha pointi 16. Stand United inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi 20 baada ya kucheza michezo 11, imeshinda mitano, sare tano na kupoteza mmoja. Hautakuwa mchezo mrahisi kwa kila mmoja, zote ni timu nzuri na zinahitaji matokeo. Majimaji itaikaribisha Ruvu Shooting.

Timu hiyo ambayo bado iko kwenye hatari ya kushuka daraja imekuwa ikijitahidi katika michezo iliyopita na kufanya vizuri. Tayari imeshinda michezo miwili, katika 11 iliyocheza na kufikisha pointi tisa. African Lyon itakuwa mwenyeji wa Mbeya City. Imetoka kufungwa na Majimaji hivyo, huenda ikalipiza kisasi kwa Mbeya.

Iwapo itashindwa kujitahidi kupata matokeo itaendelea kushuka. Imefikisha pointi 10 katika michezo 11. Ndanda inaikaribisha Mwadui FC kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona. Timu hizo zimetofautiana kwa pointi tatu. Ndanda inashika nafasi 10 kwa pointi 13 na Mwadui ya 12 kwa pointi 10. Ushindi kwa kila mmoja ni muhimu.

ZeroDegree.
Yanga, Azam majaribuni tena leo. Yanga, Azam majaribuni tena leo. Reviewed by Zero Degree on 10/22/2016 10:05:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.