Loading...

Zoezi la kuwaanika Madereva walevi mitandaoni lasitishwa.

Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga amesema wamesitisha kuwatangaza watuhumiwa katika mitandao ya kijamii baada ya kupata malalamiko ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Hata hivyo, amesema hadi wanasitisha walikuwa wamewakamata madereva 20 wa Dar es Salaam, lengo likiwa ni kuonyesha jamii ili wengine wenye tabia hiyo wajifunze kupitia kwa wenzao na kuacha kuendesha wakiwa wamelewa.

“Kwa sababu watu wengi wapo mtandaoni ilikuwa rahisi ujumbe kuwafikia kwa wakati mmoja. Tulipata malalamiko ya haki za binadamu kuwa kufanya hivyo kunawasababishia kudhalilika katika familia zao, tukaona tusitishe,” amesema Mpinga.

Hata hivyo, amesema pamoja na kusitisha utaratibu huo, madereva wasijisahau kwa sababu vijana wapo kazini na wanaendelea kuwakamata wale wote watakaokiuka sheria za barabarani, ikiwamo hiyo ya kuendesha wakiwa wamelewa.

Awali, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imelitaka Jeshi la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani, kuacha kuziweka hadharani picha za madereva wanaotuhumiwa kukiuka sheria, badala yake liwafikishe mahakamani kwanza.

Kauli ya Tume hiyo imetokana na utaratibu ulioanzishwa na trafiki wa kuwavisha mabango madereva wanaotuhumiwa kukiuka sheria ambayo yameandikwa makosa yao na kurushwa kwenye mitandao ya kijamii kabla hawajafikishwa mahakamani.

ZeroDegree.
Zoezi la kuwaanika Madereva walevi mitandaoni lasitishwa. Zoezi la kuwaanika Madereva walevi mitandaoni lasitishwa. Reviewed by Zero Degree on 12/27/2016 01:28:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.