Loading...

Ajira za walimu kutangazwa

WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Amali imesema inakusudia kutangaza ajira za walimu hivi karibuni ambapo watu watakaochaguliwa wawe tayari kufanya kazi shule yoyote watakayopangiwa.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Mmanga Mjengo Mjawiri alisema hayo wakati akizungumza na walimu wa shule ya Kigomani mjini Matemwe wakati akikabidhi msaada uliotolewa na mwekezaji wa hoteli ya Matemwe Bangalows.

Mjawiri alisema tatizo la upungufu wa walimu kwa baadhi ya shule linachangiwa na ukweli kwamba walimu wanaopangiwa kufundisha katika shule zilizopo vijijini husita kufanya hivyo kwa sababu mbalimbali.

Mjawiri alisema Wizara ya Elimu inachukua juhudi kubwa kupambana na tatizo la ajira kwa walimu, lakini baada ya muda mfupi tatizo lipo pale pale kwa sababu baadhi ya walimu wanakacha kufanya kazi katika vituo walivyopangiwa awali.

“Tunakusudia kutangaza nafasi za ajira kwa walimu, lakini masharti yetu makubwa kwanza walimu watakaochaguliwa wawe tayari kufanya kazi sehemu zenye upungufu wa walimu,” alisema.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Kigomani, Silima Mcha alisema shule hiyo inakabiliwa na tatizo la upungufu mkubwa wa vifaa vya kufundishia ikiwemo vya maabara kwa masomo ya sayansi.

Alisema tatizo hilo kwa kiasi kikubwa limedhoofisha maendeleo ya wanafunzi wa masomo ya sayansi na kushindwa kufaulu.

Mwekezaji wa Hoteli ya Matemwe Bangalow, Rose Owen alisema amekuwa mstari wa mbele kusaidia maendeleo ya jamii katika kijiji hicho ikiwemo sekta ya elimu.

Alisema katika kipindi cha miaka mitano ametoa Sh milioni 200 kusaidia maendeleo katika kijiji hicho, na yupo tayari kupokea maombi na ushauri katika eneo linalohitaji la maendeleo.

Source: Habari Leo
Ajira za walimu kutangazwa Ajira za walimu kutangazwa Reviewed by Zero Degree on 2/15/2017 02:14:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.