Loading...

Donald Ngoma hali bado tete, Vincent Bossou arejea kikosini

MSHAMBULAIJI wa Yanga, Donald Ngoma bado anaendelea kuuguza goti na ataukosa mchezo wa marudiano wa klabu bingwa Afrika dhidi ya Ngaya de Mde utakaochezwa Jumamosi ijayo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Meneja wa Yanga, Hafidh Saleh, alisema kuwa nyota huyo hawezi kuuwahi mchezo huo wa Jumamosi kwa kuwa bado ajapona goti.

Alisema nyota huyo pia hana uhakika kama atakuwa fiti kwenye mchezo wa Februari 25 dhidi ya mahasimu wao Simba.

"Ki ukweli ngoma bado hali yake haijatengemaa, hawezi kuuwahi mchezo wa Jumamosi, labda tusubiri kuelekea mchezo dhidi ya Simba na pia hakuna uhakika sana," alisema Saleh.

Hata hivyo, Saleh alisema, beki wa kati wa timu hiyo, Vincent Bossou jana alianza mazoezi na timu hiyo na anaweza akawamo kwenye kikosi kitakachoumana na klabu hiyo ya Comoro.


"Bossou leo ameanza mazoezi, na yupo fiti baada ya kukosa michezo iliyopita, ameonekana kuwa kamili na kocha (George Lwandamina) amefurahishwa na kurejea kwake," aliongeza kusema Saleh.

Aidha, Meneja huyo alisema wapinzani wao (Ngaya de Mde) wanategemewa kuwasili nchini leo kwa ajili ya mchezo huo wa marudiano.

Yanga ina kazi nyepesi kwenye mchezo huo wa marudiano baada ya kufanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 5-1 kwenye mchezo wa kwanza uliochezwa Jumamosi iliyopita nchini Comoro.

Ili Yanga itolewe, Ngaya de Mde inahitaji kushinda kwa idadi ya magoli 5-0.

Source: Nipashe
Donald Ngoma hali bado tete, Vincent Bossou arejea kikosini Donald Ngoma hali bado tete, Vincent Bossou arejea kikosini Reviewed by Zero Degree on 2/16/2017 11:55:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.