Loading...

Wabunge wa upinzani wasusia kikao cha Bunge

Wabunge wa upinzani wakitoka nje ya ukumbi wa Bunge
Wabunge wa upinzani jana walisusia kikao cha Bunge mjini Dodoma, wakipinga kile walichodai ni mhimili huo wa dola kudhalilishwa na kushushiwa hadhi yake na Jeshi la Polisi.

Tafrani hiyo iliibuka saa 10:22 jioni baada ya Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kukataa hoja ya Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT -Wazalendo), Zitto Kabwe aliyetaka Bunge lijadili na kuweka azimio la kadhia hiyo.

Wakizungumza katika viwanja vya Bunge baada ya kutoka ukumbini, wabunge hao walisema vita hiyo wataiendeleza leo asubuhi, hadi kiti cha Spika kitakapotoa msimamo wa kulinda hadhi ya mhimili huo.

Kilichowasukuma zaidi wabunge hao kutoka ni hatua ya Naibu Spika, kuwaamuru askari wa Bunge kumtoa Mbunge wa Serengeti (Chadema), Marwa Ryoba aliyekuwa akipinga uamuzi wa kiti.

Baada ya uamuzi wa Naibu Spika kukataa Bunge lisijadili hoja ya Zitto na kuweka azimio, wabunge wa upinzani walionekana kupinga kwa kupaza sauti zao akiwamo Ryoba.

“Mheshimiwa Ryoba naomba utoke mwenyewe. Mheshimiwa Ryoba naomba utoke mwenyewe,” alisikika Naibu Spika akisema huku Ryoba akisema hatoki ndipo Tulia akaagiza polisi wamtoe.

Hata hivyo, wabunge wa upinzani kwa umoja wao ndipo wakaamua kutoka ukumbini na kuwaacha wa CCM wakiendelea na kikao cha Bunge cha jioni.

Kiini cha sakata hilo ni hatua ya polisi kumkamata Mbunge wa Singida Mashariki, (Chadema) Tundu Lissu, juzi jioni wakati akitoka bungeni na jana ilidaiwa polisi walikuwa wakimwinda Zitto.
Wabunge wa upinzani wasusia kikao cha Bunge Wabunge wa upinzani wasusia kikao cha Bunge Reviewed by Zero Degree on 2/08/2017 09:28:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.