Loading...

Zawadi ya aliyekuwa mshindi wa shindano la "Miss Tanzania 2016" yabadilishwa

WAKATI mrembo wa Taifa, Diana Charles "Miss Tanzania 2016" akiwa anapigwa danadana kuhusu zawadi yake ya gari baada ya kuibuka mshindi katika shindano hilo, taarifa zinaeleza kuwa zawadi atakayopewa sasa imebadilishwa.

Mchakato wa kutaka kukabidhi zawadi hiyo umekuja siku mbili baada ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kutoa tamko lake bungeni kuwa wanataka mrembo huyo apewe zawadi yake kabla ya waandaaji hawajazuiwa kibali cha kuandaa shindano hilo.

Diana alisema kuwa ameelezwa na kamati inayosimamia shindano hilo kuwa sasa atapewa gari aina ya Suzuki Swift badala ya Vitz ambayo alionyeshwa na kupiga nayo picha muda mfupi baada ya kutangazwa mshindi.

Diana alisema anashangaa na haelewi kilichosababisha zawadi hiyo kubadilishwa hali ya kuwa aliposhinda taji hilo Oktoba 29, mwaka jana alionyeshwa gari aina ya Vitz na kuambiwa atakabidhiwa baada ya utaratibu wa usajili kukamilika.



"Kwanza ilikuwa nikabidhiwe Jumanne, baadaye nikaambiwa Jumatano na leo (jana) nimeambiwa nitakabidhiwa kesho (leo) Alhamisi," alisema mrembo huyo mwenye asili ya Kimasai ambaye pia ni Lete Raha Miss Kinondoni. 

Aliongeza kuwa tayari alishakabidhiwa zawadi ya fedha Sh. milioni mbili ambazo zilitolewa mapema mwaka huu na mmoja wa wadhamini wa shindano hilo.

Alisema warembo wenzake waliofika hatua ya tano bora pia bado wanadai fedha kutoka kwa Kamati ya Miss Tanzania ambao ni pamoja na Grace Malikita aliyeshika nafasi ya pili na mshindi wa tatu Maria Peter.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Lino International Agency, 
Hashim Lundenga ambao ni waandaaji wa shindano hilo alitafutwa, ili kutoa ufafanuzi wa madai hayo hakupokea simu.
Zawadi ya aliyekuwa mshindi wa shindano la "Miss Tanzania 2016" yabadilishwa Zawadi ya aliyekuwa mshindi wa shindano la "Miss Tanzania 2016" yabadilishwa Reviewed by Zero Degree on 5/11/2017 11:28:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.