Loading...

Viwanja zaidi ya 10,000 vyawekwa sokoni Dodoma

Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma, Godwin Kunambi
MANISPAA ya Dodoma imetangaza kuanza kuuza viwanja 10,864 vilivyopo maeneo ya Mtumba na Lyumbu huku watakaoomba kununua viwanja hivyo wakitakiwa kulipa malipo yote ndani ya mwezi mmoja.

Aidha, wananchi watakaofanya ujanja ujanja kupata viwanja vingi wamewekewa mfumo wa kudhibiti hali hiyo. Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma, Godwin Kunambi alisema uunzaji huo utaanza Aprili 20, mwaka huu. Viwanja vinavyotarajiwa kuuzwa ni miongoni mwa viwanja 19,467 vilivyopimwa na kukamilika baada ya kazi ya upimaji iliyoanza Januari mwaka huu hadi sasa na idadi ya viwanja vilivyopimwa kwenye mabano kuwa ni Iyumbu (967), Mtumba (9,897), Michese (1,500) na Nala (7,000). Mradi unaogharimu zaidi Sh bilioni 44.32.

Akitoa mchanganuo wa bei ya viwanja kwa mita ya mraba moja, Kunambi alisema eneo la Mtumba viwanja vimegawanywa katika kanda tatu; ambao ukanda wa barabarani kiwanja cha makazi kitauzwa Sh 8,000, makazi na biashara Sh 8,500, biashara Sh 10,000, taasisi Sh 7,000 na viwanda vidogo Sh 20,000. Alisema eneo la kati Mtumba, kiwanja cha makazi ni Sh 6,000, makazi na biashara Sh 7,500, biashara Sh 8,000, taasisi 5,000 na viwanda vidogo ni Sh 15,000; huku ukanda wa barabara ya Kikombo, kiwanja cha makazi ni Sh 3,000, makazi na biashara Sh 5,500, biashara Sh 6,000 na viwanda vidogo Sh 10,000. Kunambi alisema eneo la Iyumbu viwanja vya makazi vitauzwa Sh 6,000, makazi na biashara Sh 8,000, biashara Sh 15,000, taasisi Sh 7,000 na viwanda vidogo Sh 20,000.
Viwanja zaidi ya 10,000 vyawekwa sokoni Dodoma Viwanja zaidi ya 10,000 vyawekwa sokoni Dodoma Reviewed by Zero Degree on 4/14/2018 11:05:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.