Loading...

Molinga kumtoa nishai Matola leo


Straika wa mwisho kusajiliwa na Yanga, David Molinga ameapa kumtoa nishai, Seleman Matola wa Polisi Tanzania ambaye, hajawahi kuifunga Yanga Jijini Dar es Salaam akiwa na timu za mkoani.

Licha ya kwamba leo atamkosa kipa wake namba moja, rekodi zinaonyesha kwamba tangu akiwa na Lipuli amecheza mechi nne za dhidi ya Yanga na moja ya FA.

Lakini kwenye mitandao ya kijamii jana, viongozi wa Yanga walianzisha zengwe kwamba baadhi ya viongozi wa Simba walionekana kwenye kambi ya Polisi iliyokuwa ufukweni, lakini Simba walikanusha.

Matola ambae enzi zake alikuwa kiungo, akiwa na Lipuli amecheza dhidi ya Yanga mara tano, akaambulia sare na kipigo kimoja Dar es Salaam na Iringa akaambulia ushindi mara mbili na mkong’oto mmoja. Pia walipokutana katika Kombe la Shirikisho (FA) akiwa Lipuli alishinda mabao 2-0 nyumbani.

Akiwa na Polisi Tanzania ambayo inashiriki ligi kuu kwa mara ya kwanza msimu huu, aliifunga Yanga mabao 2-0 katika mechi ya kirafiki mjini Moshi huku Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera akidai alikuwa akitesti mitambo.

Katika mechi ya leo Yanga itamkosa Zahera ambaye ataanza kutumikia adhabu ya kufungiwa mechi tatu.

Yanga ambao hawana pointi yoyote ile kwenye ligi watacheza mechi hiyo ya ligi ikiwa ya pili, ambayo itapigwa saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Uhuru ikiwa ni kisasi na kuonyeshana ubabe.

Matola ambaye ni mchezaji aliyeichezea Simba na kuikochi kwa mafanikio, hutoa ushindani mkubwa kila anapokutana na Yanga jambo ambalo linaongeza msisimko kwenye mechi ya leo.

Hii itakua mara ya pili kwa Matola kuwa Dar es Salaam akisaka pointi tatu lakini inaonyesha jiji hili siyo rafiki kwao.

Mechi ya kwanza ambayo walicheza na Ruvu Shooting walichakazwa kwa bao 1-0 ikiwa ni mechi ya kwanza waliyoicheza nje ya mkoa wao wa Kilimanjaro.

Leo watakuwa na kibarua kingine cha kujaribu kujisafisha lakini wapembuzi wa mambo wanaiona nafasi yao kuwa finyu kutokana na hasira za Yanga baada ya kutolewa kimataifa huku straika, David Molinga akisisitiza kuanza rasmi ligi leo.

Zahera baada ya kuondolewa Ligi ya Mabingwa Afrika ametamba kwamba sasa nguvu zao wanaelekeza kwenye ligi kwa ajili ya kujinasua na nafasi ambayo wapo katika ligi hadi sasa

Wachezaji wanne wa Yanga Paul Godfrey ‘Boxer’, Mohammed Issa ‘Banka’, Juma Mahadhi na Raphael Daud wataukosa mchezo wa leo dhidi ya Polisi Tanzania kutokana na kuwa majeruhi.

Ofisa habari wa Yanga, Hassan Bumbuli alisema kuwa wachezaji hao wanne watakosekana kutokana na majeruhi pamoja na kocha, lakini Balama Mapinduzi na Issa Bigirimana watakuwepo baada ya kupona majeraha yao.

Mhamasishaji wa Yanga, Antonio Nugaz ameliambia Spoti Xtra, mshambualiaji wao David Molinga ameapa kuanza ligi siku hiyo akiahidi ushindi mnono huku kiungo Abdulaziz Makame akisema kuwa hatafanya makosa mengine ndani ya Yanga na kuwaomba mashabiki wajitokeze katika mchezo huo.

“Nimeongea na Molinga ameniahidi ushindi mnono ambapo aliniambia kuwa ataanza kuonyesha cheche zake katika mchezo wa leo huku Makame akiniahidi kutofanya tena makosa hivyo mashabiki mjitokeze kwa wingi,” alisema Nugaz.

“Tumejiandaa vyema kuelekea mchezo wetu dhidi ya Yanga, tunahitaji kuendeleza rekodi katika mechi za maandalizi ya ligi, tuliwafunga naamini tukijipanga na kujituma tutafanikiwa kushinda.

“Mechi itakuwa ngumu, wenzetu pia wanahitaji kuona wanashinda, wachezaji wanaonyesha muamko wa hali ya juu, wote wapo vizuri isipokuwa kipa wangu namba moja Yusuph Mohammed amepatwa na majeruhi juzi yaliyomlazimu kutofanya mazoezi,” alisema Matola mchezaji wa zamani wa Super Sport ya Afrika Kusini.

Polisi Tanzania wamesema kuwa wachezaji wake wote leo wataogelea minoti na zawadi za kutosha endapo wataifunga timu ya Yanga ambayo mlinda mlango wao namba moja ni Metacha Mnata.

Afisa Habari wa Polisi Tanzania, Frank Lukwaro alisema; “Tunajua tunacheza na timu ngumu na kubwa jambo lililotufanya tuwaandae wachezaji wetu kisaikolojia na wanatambua kwamba kuna zawadi zao na bonasi ambazo tutawapa wakishinda.”
Molinga kumtoa nishai Matola leo Molinga kumtoa nishai Matola leo Reviewed by Zero Degree on 10/03/2019 08:50:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.