Loading...

Mama ADAIWA KUMUOZESHA binti yake wa miaka 13.


Waziri wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

Dodoma. Wakati Serikali na wadau mbalimbali wa watetezi wa haki za wanawake na watoto wakihimiza elimu kwa mtoto wa kike, mama mmoja mkoani hapa anatuhumiwa kutaka kumuozesha mtoto wake mwenye miaka 13 (jina linahifadhiwa) baada ya kupokea mahari ya Sh600,000 na ng’ombe wanne.

Tukio hilo lilitokea leo katika Mtaa wa Chikole, Kata ya Msalato Manispaa ya Dodoma.

Mama huyo anadaiwa kutaka kumfungisha ndoa binti huyo kwa kijana mmoja anayeishi mtaani hapo.

Hata hivyo, mpango huo wa ndoa ulitibuliwa na Mwenyekiti wa Mtaa huo, Nashoni Chinywa ambaye baada ya kupata taarifa aliamua kuwaita polisi wauzuie.

Akizungumzia tukio hilo, mama wa mtoto huyo, Mdala Mazengo alisema aliamua kumuozesha binti yake baada ya kumtaarifu kuwa amepata mchumba.

Naye mtoto huyo alidai kukutana na kijana huyo mwenye umri wa miaka 20 mtaani hapo na kumuahidi kufunga naye ndoa.

Hata hivyo, baadhi ya majirani walidai kuwa mama huyo ambaye ni mjane, ana tabia ya kuwaozesha watoto wake wa kike wakiwa na umri mdogo.

Chinywa alisema baada ya mahojiano, mama huyo alikiri kufanya kosa hilo baada ya kuchoshwa na tabia za watoto hao kwani hata dada yake alibebeshwa mimba akiwa nyumbani.

Hata hivyo, alisema kuwa hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa baada ya Kamati ya Serikali ya Mtaa kukutana na Kamati ya Maendeleo ya Jamii kujua ni hatua gani zichukuliwe dhidi ya mama huyo.

“Alikataa shule, sasa yeye mwenyewe aliniambia amepata mchumba na mimi niliamua kumuozesha kwa kuwa wao wenyewe wamependana,” alisema Mdala Mazengo na kuongeza:

“Walishatoa barua ya posa na kesho ndiyo tulikuwa tunapanga mahari ya kulipa, wao walikuwa wanataka kunipa mahari kidogo, sasa wakati tunabishana ndipo mwenyekiti na maaskari wakafika hapa nyumbani na kutukamata.” Walidai kuna mtoto mwingine alimuozesha akiwa na miaka 14.



Source: Mwananchi
Mama ADAIWA KUMUOZESHA binti yake wa miaka 13. Mama ADAIWA KUMUOZESHA binti yake wa miaka 13. Reviewed by Zero Degree on 1/13/2016 01:17:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.