Loading...

Tamko zito lafuatia, baada ya mazishi ya MENEJA WA ZANTEL aliyeuawa kwa kupigwa risasi.


Jeneza lililobeba mwili wa marehemu likiwa Kanisani kwa ajili ya kuombewa.

DAR ES SALAAM: Tamko zito limetolewa na waombolezaji kufuatia kifo cha bosi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja wa Kampuni ya Zanzibar Telecom Limited (Zantel), Gabriel Kamukara, 39, (pichani) kuuawa kwa kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi.

Kamukara alipigwa risasi Desemba 22, mwaka jana eneo la Barabara ya Cocacola jijini Dar na kuporwa shilingi milioni 10 alizotoka kuzichukua benki.

Baadhi ya waombolezaji kwenye msiba huo, nyumbani kwa marehemu, Mbezi Beach, Dar walisema vifo vya wateja wa mabenki kupigwa risasi wakitoka kuchukua fedha vimekuwa vikiongezeka kila siku kuliko vya wateja wanaopeleka fedha benki.

Mke wa marehemu akiuaga mwili wa mumewe kwa simanzi kubwa.

“Mimi natoa tamko! Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, Ernest Mangu afuatilie kuona tatizo liko wapi! Ukimuuliza kila mtu anasema baadhi ya wahudumu wa mabenki wanahusika.

“Wao ndiyo wanawajulisha majambazi kwamba mtu anayetoka kavaa hivi, kabeba begi f’lani, ana kiasi f’lani cha fedha. Ndiyo maana wengi wanapigwa risasi wakitoka kuchukua fedha,” alisema mwombolezaji huyo aliyejitambulisha kwa jina la Johnson Kimaki, mkazi wa Mbezi.




Waombolezaji wakiaga mwili wa marehemu.

Mwombolezaji mwingine, Anna Mwakole, alisema: “Niliwahi kumwona keshia mmoja wa benki moja hapa Dar akimhudumia mteja anayechukua fedha nyingi huku akiandika meseji kwenye simu. Ilinitia wasiwasi. Haiwezekani majambazi wakajua anayetoka benki ana pesa nyingi, wanaambiwa.

“Sijawahi kusikia mteja kapigwa risasi akiwa ametoka kuchukua shilingi laki 2. Lazima iwe mamilioni. Serikali ifumbue macho hapa. Sheria zinakataza makeshia kuwa na simu kaunta, lakini hazizingatiwi.”



Akizungumzia tukio hilo, mdogo wa marehemu, Migration Kamukara, alisema siku ya tukio marehemu alitoka kazini saa nne asubuhi, akaenda kufungua kinywa kisha akaenda benki na kukumbwa na mauti.

“Saa tano asubuhi nilipigiwa simu, nikaambiwa kaka ameuawa kwa kupigwa risasi na majambazi na wamempora fedha akitokea benki. Zilikuwa ni fedha kwa ajili ya ujenzi.
“Sijajua hao watu walitumwa au walimfuatilia tu maana walikuwa wawili na bodaboda. Walimfyatulia risasi ya mkononi na kifuani, akafariki dunia papo hapo.


Marehemu Gabriel Kamukara enzi za uhai wake.

Ibada ya kuuaga mwili wa marehemu ilifanyika katika Kanisa la Mtakatifu Petro Oyster Bay, Dar na kuzikwa Makaburi ya Kinondoni jijini huku wengi wakipoteza fahamu mara kwa mara. Marehemu ameacha mjane na watoto wawili.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, ACP Camillius Wambura amesema atahakikisha waliohusika na tukio hilo wanakamatwa.
Imeandaliwa: Makongoro Oging’ na Mayasa Mariwata.


Source: GPL

Comment & Share this story!!
Tamko zito lafuatia, baada ya mazishi ya MENEJA WA ZANTEL aliyeuawa kwa kupigwa risasi. Tamko zito lafuatia, baada ya mazishi ya MENEJA  WA ZANTEL aliyeuawa kwa kupigwa risasi. Reviewed by Zero Degree on 1/05/2016 10:48:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.