Loading...

Waziri Mkuu atinga ghafla Hospitali ya Mawenzi Kilimanjaro.


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika moja ya ziara zake.

Moshi. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amefanya ziara ya kushtukiza kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro, Mawenzi na kubaini vyumba viwili vya upasuaji havitumiki.

Akiwa katika chumba cha upasuaji na Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Bingileki Lwezaula, alibaini kuwapo vyumba vitatu vya kutoa huduma hiyo lakini kinachotumika ni kimoja.

Hata hivyo, alielezwa kuwa vingine havitumiki kwa kuwa havina dawa za kulaza wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji.

Waziri Majaliwa, pia alitembelea wodi ya utabibu ya wanawake na kupokea malalamiko kutoka kwa wagonjwa kuhusu kukosekana kwa dawa hospitalini hapo. 

Ofisa Muuguzi wa wodi hiyo, Anjela Mwakalile alisema wametuma maombi ya kupatiwa dawa kutoka Bohari ya Dawa (MSD) lakini bado hazijafika.

“Kwa nini hamuwezi kuagiza dawa nyingi kwa magonjwa ambayo mnajua yanajirudia mara kwa mara ili wagonjwa wasipate usumbufu?

“Hii ni hospitali ya mkoa na mgawo wa dawa unaopaswa kuja hapa ni kwa kiwango cha mkoa.  
Haiwezekani, mnafanya hivyo ili wagonjwa wajinunulie dawa kutoka kwenye maduka yenu?” alihoji Waziri Mkuu. 

Wakati akitoka wodi ya watoto, kijana mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Bakari Hussein alimweleza Waziri Mkuu kwamba dawa pekee wanayopatiwa kwenye hospitali hiyo ni paracetamol.

“Dawa nyingine zote unaandikiwa ukanunue maduka ya nje. Na ukizipata ni kwa bei kubwa,” alisema Hussein.

Waziri Mkuu alimwagiza Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Severine Kahitwa apeleke maombi ya kupatiwa mafundi wa mashine za x-ray haraka iwezekanavyo kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Waziri Mkuu amefikia uamuzi huo baada ya kukuta mashine kubwa kwenye chumba cha mionzi cha hospitali haifanyi kazi na inayofanya kazi ni ndogo.

Mkuu wa Kitengo cha Radiolojia, Dk Ephraim Minja alisema, “Vifaa hivyo vikipatikana vitaweza kutatua tatizo lililopo.”



ZeroDegree.
Waziri Mkuu atinga ghafla Hospitali ya Mawenzi Kilimanjaro. Waziri Mkuu atinga ghafla Hospitali ya Mawenzi Kilimanjaro. Reviewed by Zero Degree on 2/01/2016 05:26:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.