Loading...

Bibi adaiwa kumuuza mjukuu wake mwenye ulemavu wa ngozi [ Albino ].


MTOTO mwenye ulemavu wa ngozi (albino) mwenye umri wa miaka mitatu, mkazi wa wilaya ya Itilima, mkoani Simiyu hivi karibuni amenusurika kuuawa kwa kukatwa mapanga, baada ya bibi yake kudaiwa kumuuza kwa wauaji hao ili waweze kuchukua sehemu ya viungo vyake.



Mtoto huyo alinusurika kifo baada ya wauaji hao kufika nyumbani kwao majira ya jioni na kumkuta akiwa na mama yake mzazi na ndipo wakamkwapua na kutaka kukimbia naye, lakini mama yake akafanikiwa kumuokoa baada ya kupambana na kunyang’anyana hadi kusababisha mtoto huyo kuchubuka mkono mmoja.

Hayo yalielezwa juzi na Mkurugenzi wa Kituo cha Kulelea Watoto wa makundi Maalumu cha Bikira Maria Mama wa Mungu Msaada Daima, Sista Maria Hellena, kwenye maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika juzi katika kata ya Lamadi, wilayani hapa.

“Hao wauaji walifika nyumbani kwao na mtoto huyo na kumkuta akiwa na mama yake mzazi, sasa wakamkwapua na kuanza kunyang’anyana, mama mtoto alifanikiwa kumuokoa mikononi mwa watu hao, lakini ngozi ya mkono ilichubuka sana ndipo wakamleta hapa na tunaendelea kumlea hapa kituoni,” alisema Sista Hellena.

Aidha, Sista Hellena alisema bibi wa mtoto huyo na wauaji hao walitoroka na kesi iko Polisi.

Katika hatua nyingine, Sista Hellena alisema kuwa watoto wengi wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya kikatili na wazazi wao, na kusema kama wanashindwa kuwalea baada ya kuwazaa ni bora wawapeleke kwenye kituo chake, hata kwa kuwatelekeza nje ya kituo hicho ili aweze kuwachukua.

Mratibu wa Kituo hicho, Belensi China, alisema watoto wanakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwa ni pamoja na kupewa kazi ngumu ya kuchunga mifugo.


ZeroDegree.
Bibi adaiwa kumuuza mjukuu wake mwenye ulemavu wa ngozi [ Albino ]. Bibi adaiwa kumuuza mjukuu wake mwenye ulemavu wa ngozi [ Albino ]. Reviewed by Zero Degree on 6/19/2016 12:24:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.