Loading...

Simba yaishika pabaya Yanga.

SIMBA washindwe wenyewe Oktoba mosi, mwaka huu kwani kwa jinsi ilivyo kwa sasa, wanaonekana kuwa imara kuanzia ndani hadi nje ya uwanja kuelekea pambano la kukata na shoka la Ligi Kuu Tanzania Bara baina yao na watani wao wa jadi, Yanga kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Zikiwa ni siku chache kabla ya pambano hilo, tayari homa imeanza kupanda miongoni mwa mashabiki wa pande zote mbili, kila mmoja akitamba kuibuka kidedea siku hiyo.

Kwa kutambua umuhimu wa mchezo huo, si tu katika kusaka pointi tatu, bali pia kulinda heshima baina ya watani hao wa jadi, Yanga jana walitua kisiwani Pemba, Zanzibar kujiwinda kwa mtanange huo wa aina yake.

Simba wanaoongoza ligi hiyo wakiwa na pointi 16 baada ya kushuka dimbani mara sita, wakifuatiwa na Stand United wenye pointi 12 ndani ya mechi sita, wamekimbia kujichimbia mjini Morogoro ili kujinoa zaidi kulipiza kisasi cha msimu uliopita cha kutambiwa na watani wao hao.

Yanga wapo nafasi ya tatu na pointi zao 10, wakiwa wamecheza mechi tano tu, wakifuatiwa na Azam wenye pointi 10 baada ya kushuka dimbani mara sita.

Pamoja na timu zote hizo kuupania mchezo huo, Simba ndio wanaoonekana kujipanga zaidi kuliko wapinzani wao hao wa jadi jambo ambalo linaweza kuwapa matokeo mazuri tofauti na msimu uliopita walipokubali kufungwa michezo yote miwili mabao 2-0.

Wekundu wa Msimbazi hao katika mechi zao zote sita zilizopita, wameonyesha kandanda la kuvutia ndani ya uwanja, huku safu zao zote kuanzia ile ya ulinzi, kiungo hadi ushambuliaji zikionekana kuwa imara.

Ukiachana na hilo, Simba wana faida nyingine inayowapa nafasi ya kushinda mchezo huo kutokana na jinsi viongozi, wanachama na mashabiki wake walivyojipanga nje ya uwanja.

Katika upande huo, wale wote waliokuwa wameipa kisogo timu yao misimu kadhaa iliyopita, wamerudi kundini na kuamua kwa kauli moja kuungana kwa hali na mali kuhakikisha Yanga wanakiona cha moto Jumamosi.

Ili kuhakikisha hilo linatimia, wanachama wenye mapenzi ya dhati na Simba, kuanzia mashabiki na wanachama wa kawaida, wabunge, mawaziri, viongozi na matajiri mbalimbali, wameamua kuchanga fedha za kuwapa wachezaji iwapo watashinda mchezo huo, ikiwamo kununua mabao yote watakayofunga kila moja kwa dau nono.

Pia wanachama hao ambao wengine ni wale waliowahi kushika nyadhifa tofauti Msimbazi, wakiwamo aliyewahi kuwa Mwenyekiti, Hassan Dalali; Mbunge wa Ilala, Idd Azan Zungu; Mfanyabiashara maarufu nchini, Mohammed Dewji ‘Mo’, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Zacharia Hanspoppe, Katibu Mkuu wa zamani, Kassim Dewji (KD) na wengineo wengi, wamekuwa wakihamasishana kufanya kila linalowezekana ili watoke uwanjani na ushindi Jumamosi.

Katika michezo iliyopita msimu huu, wachezaji wa Simba wamekuwa wakipewa Sh milioni 10, jambo ambalo limekuwa likiwapa morali ya kucheza kufa au kupona ili kupata matokeo mazuri.

Ndani ya misimu takribani minne iliyopita, Simba wamekuwa na migogoro ya mara kwa mara iliyosababisha kuwapo kwa makundi, likiwamo lile la Simba Ukawa, hali iliyosababisha kudorora kwa timu yao kwenye Ligi Kuu Bara na hivyo kukosa nafasi ya kushiriki michuano ya kimataifa.

Lakini kwa sasa mambo yanaonekana kuwa mazuri Msimbazi, jambo linalotajwa kama silaha kubwa ya ushindi kwa Wekundu hao wa Msimbazi msimu huu.

Halikadhalika, Simba wamefanikiwa kumnasa Patrick Kahemele aliyepewa nafasi ya Katibu Mkuu wa klabu hiyo, akiwa ni mchapakazi anayeijua vema kazi yake, huku Yanga wao wakiwa na pengo la kuondokewa na aliyekuwa akishikilia cheo kama hicho, Jonas Tiboroha, ambaye alikuwa mtu muhimu mno katika kupanga mikakati ya ushindi kuanzia ndani hadi nje ya uwanja.

Ukiachana na yote hayo, kuelekea mchezo huo wa Jumamosi, Simba wanajivunia rekodi yao ya kutopoteza mchezo wa ligi, wakiwa wamepata sare moja tu, huku wakitoka katika ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Majimaji mwishoni mwa wiki iliyopita, wakati Yanga wakiwa wametoka kupokea kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Stand United, mjini Shinyanga.

Kwa hali kama hiyo, ni wazi kuwa iwapo hakutaingia ‘kidudu mtu’ Msimbazi kabla ya Jumamosi, ni wazi kuwa Wekundu wa Msimbazi hao watakuwa na nafasi kubwa ya kuibuka na ushindi kwa jinsi kikosi chao kilivyotulia uwanjani, huku nje kukiwa na sapoti ya nguvu kutoka kwa wanachama mafundi wa ‘fitna’ wa klabu hiyo wakiongozwa na KD.

Source: Bingwa

ZeroDegree.
Simba yaishika pabaya Yanga. Simba yaishika pabaya Yanga. Reviewed by Zero Degree on 9/27/2016 10:09:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.