Loading...

Tathimini ya vita ya kushuka daraja Ligi Kuu ya Uingereza [EPL]

ZIKIWA zimesalia mechi 13 kuhitimishwa kwa Ligi Kuu nchini England (EPL), vita ya nani anabaki kwenye ligi hiyo msimu ujao, imekuwa kubwa na haitabiriki na ngumu kuliko miaka mingine.

Ushindi wa Swansea dhidi ya mabingwa watetezi, Leicester umedhihirisha kwamba timu sasa zimefufuka na kuonyesha kwamba, kuwa bingwa mtetezi wa EPL si sababu ya kutoshuka daraja.

Timu tano zilizoko mkiani zinatakiwa kushinda mechi zao saba zikiwamo za wao kwa wao katika mechi 10 zilizosalia, hali inayomaanisha kwamba vita ya kushuka daraja haina mwenyewe na lolote linaweza kutokea kwa timu yoyote kati ya hizo.

Makala haya yanaangalia timu hizo na kuona nini kinaweza kuzitokea EPL msimu huu kulingana na mechi zilizobakia na nafasi inazoshika kuanzia nafasi ya 14.
FC Bournemouth

Ina jumla ya pointi 26, tofauti ya mabao -12

Nini kinaendelea?

Kwa nafasi hiyo wanaonekana wako salama, lakini Bournemouth wananyooshewa kidole katika nafasi za kushuka daraja kutokana na mwenendo wao wa hivi karibuni, kwani wameshinda mechi moja tu kati ya nane walizocheza hivi karibuni kwenye EPL.

Wamepata pointi tano tu kati ya 24 walizotakiwa kupata, na hii ni mbaya sana na kama hawatarekebisha wanaweza kujikuta wakishuka bila kutarajia.

Bournemouth wanacheza soka safi sana, lakini ukuta wao umekuwa laini mno kiasi cha kuruhusu wapinzani kupita kirahisi.

Wana sababu za kuwa na matumaini?

Eddie Howe ni kocha chipukizi na timu yake inaweza kutoa upinzani mkali na usiotarajiwa kwa timu yoyote katika EPL, wanabadilika kulingana na mchezo, hilo linaweza kuwapa matumaini.

Wana sababu ya kuhofu?

Mwenyendo wao wa kuruhusu mabao ya kipuuzi ni alama kwamba hawako salama. Wameruhusu mabao zaidi ya matatu au zaidi katika mechi moja kwenye mechi zao za hivi karibuni.

Ratiba yao inasemaje?


Wana mechi dhidi ya Middlesbrough, Sunderland, Stoke, Burnley na mabingwa watetezi Leicester na kama watashinda anagalau mechi tatu kati ya hizi za mwishoni watapata matumaini.
Swansea

Wao wana pointi 24 huku wakiwa na tofauti ya mbao -23


Nini kinaendelea?


Francesco Guidolin na Bob Bradley wameonyesha mlango wa kutokea kwenye klabu hiyo hasa baada ya kuonekana wazi Swansea imekosa namna ya kujinasua kutokana na kushuka daraja.

Ujio wa kocha mpya, Paul Clement, umeanza na matokeo mazuri kwa vijana hao na kurejesha matumaini hasa baada ya ushindi wa mechi nne kati ya sita walizocheza hivi karibuni ikiwamo ule wa dhidi ya mabingwa watetezi.

Wana sababu ya kuwa na matumaini?


Swansea walijiweka vyema sana chini ya Clement ambaye amewaibuwa vijana watano wapya kikosini wakiwemo washambuliaji wawili ambao wamekuwa wakifunga mabao.

Wana sababu ya kuwa na hofu?


Kama Gylfi Sigurdsson au Fernando Llorente watapata majeraha, basi litakuwa tatizo kubwa kwa Swansea na litaathiri sana katika jitihada zao za kujitanua kutokana na kushuka daraja.

Ratiba yao ikoje?


Wana safari ya kwenda nyumbani kwa vinara wa ligi hiyo, Chelsea, kichapo kutoka kwa miamba hiyo ya Darajani inayofukuzia ubingwa kinaweza kuwavuta. Wataikaribisha Tottenham inayoshika nafasi ya tatu, nao wanaweza kuwatibua, lakini mbele yao tena watalazimika kwenda Old Trafford kuwavaa Manchester United. Wanatakiwa kuvuna pointi angalau tatu kwenye mechi hizo tatu mbele ya vigogo hao waliopo kwenye sita bora. Mtihani uko hapo.
Middlesbrough

Wana pointi 22 na tofauti ya mabao -8

Nini kinaendela?


Haifurahishi sana. Middlesbrough hawafungi mabao mengi lakini pia hawaruhusu kufungwa, hii ndiyo ishara nzuri kwa kikosi cha Aitor Karanka, timu ina jumla ya mabao 46, imefunga 19 na kufungwa 27, wakiwa wamefungwa mabao machache zaidi kati ya timu zilizo kwenye vita ya kushuka daraja.

Mashabiki wamekosa imani na Karanka ambaye mechi yake ya mwisho kushinda ni ya Desemba 17, mwaka jana zaidi ya mechi tisa zilizopita.

Wana matumaini?


Boro ndio timu yenye ukuta mzuri kati ya timu zinazopangana kushuka daraja, wamefungwa mabao 27 tu na juu yao katika kufungwa mabao, wapo Chelsea na Tottenham walifungwa mabao 18 na Man United wakifungwa mabao 21. Wakinoa kidogo safu ya ushambuliaji maana yake wanaweza kusalimika.

Nini kinawapa hofu?


Boro hawana safu kati ya ushambuliaji, wamefunga mabao 19 tu, ubutu wa safu hii ya ushambuliaji unaweza kuwaumiza na pengine ndio hofu yao kubwa katika vita hii isiyokuwa na mwenyewe.

Ratiba yao ikoje?


Vijana hawa wa Karanka ni lazima wapate ushindi mbele ya wapinzani wao kwenye vita hiyo, Crystal Palace, Swansea, Sunderland na Hull mechi ambazo zinakuja Aprili kabla ya kuanza kibarua kigumu mbele ya Arsenal, Manchester City, Chelsea na Liverpool; mechi ambazo zitakuwa mwishoni mwa msimu. Ni ratiba ngumu sana.
Leicester

Wana pointi 21 na tofauti ya mabao -19

Nini kinaendelea?


Nani anayejua kinachoendelea ndani ya vyumba vya kubadilishia nguo vya timu hii? Pengine wataweka rekodi iliyowekwa na Manchester City mwaka 1930 ya kutoka kuwa Bingwa hadi kushuka daraja.

Takwimu zao zina viashiria vyote. Imekuwa timu ya kwamza inayoshikilia taji na kupoteza mechi tano mfululizo tangu Machi mwaka 1956, wakati Chelsea walipofanya hivyo. Na wameshindwa kupata mabao katika dakika 610 walizocheza ambazo ni sawa na saa 10 na dakika 10 ambazo pia ni sawa na wastani wa mechi sita.

Wana matumaini?

Leicester ina wachezaji wengi wale wale walioipa ubingwa na ni wale wale ambao waliinusuru kutokana na kushuka daraja misimu miwili iliyopita kabla ya kuchukua ubingwa. Wana matumaini kuna vitu vitabadilika katika mechi zilizosalia.

Nini kinawapa hofu?


Hali kama hii ilishawahi kuwakuta wakiwa na Nigel Pearson na kama hawatakuwa makini, bila shaka wanaweza kujikuta kwenye wakati mgumu zaidi kubaki Premier msimu huu.

Ratiba yao ikoje?


Liverpool na Arsenal ni miongoni mwa timu watakazocheza nazo kwenye mechi tatu zinazofuata. Hapa Claudio Ranieri anatakiwa kukaza mkanda kweli kweli kabla hajasafiri kuwafata Hull City kwenye mchezo unaotabiriwa kuwa mgumu zaidi kwao.
Hull City

Wana pointi 20 na tofauti ya mabao 27

Nini kinaendelea?


Walianza msimu kwa kusuasua chini ya Mike Phelan, lakini ujio wa Marco Silva umeonekana kuibadilisha kabisa Hull.

Mreno huyu amerejesha hali ya kujiamini kwenye kikosi na sasa wamekuwa wapambanaji wa kweli wanaopigana kutoshuka daraja.

Dirisha dogo waliwauza Jake Livermore na Robert Snodgrass lakini usajili waliofanya ukakiimarisha kikosi chao. Ushindi dhidi ya Liverpool umekuja wakati sahihi kwao kwenye vita ya kusalia EPL msimu huu.

Nini kinawapa hofu?

Silva anaonekana mtu sahihi kwao, ana mipango imara na kuna uhakika upo ndani ya mashabiki wao wanaomsapoti, lakini kwa sasa ushindani ni mkubwa kwa timu za chini, hivyo hawatakiwi kupoteza mchezo wowote kutoka sasa.

Ratiba yao ikoje?

Dhidi ya Burnley, nyumbani, ugenini dhidi ya Leicester na nyumbani tena dhidi ya Swansea, hii ndiyo michezo itakayoweza kutoa taswira ya Hull msimu huu kwenye EPL.
Crystal Palace

Wana pointi 19 na tofauti ya mabao 14

Nini kinaendelea?


Vile ilivyotarajiwa kuwa wakati Sam Allardyce akipewa timu inaonekana kuwa tofauti kidogo, wameshinda mchezo mmoja tu dhidi ya Bournemouth katika mechi nane walizocheza.

Kichapo cha 4-0 walichokipata dhidi ya Sunderland na kile cha bao 1-0 dhidi ya Stoke, ni ishara kuwa Big Sam ana kazi kubwa ya kufanya ili kuinusuru Palace isiteremke daraja msimu huu.

Nini kinawapa hofu?

Klabu inaonekana kukosa umoja na wachezaji wanacheza kwa vipaji binafsi, hali hii itawapa wakati mgumu kama wanahitaji kusalia kwenye Premier msimu huu.

Ratiba yao ikoje?

Wana ratiba ngumu sana, watacheza dhidi ya Tottenham, Chelsea, Arsenal, Liverpool, Manchester City na Man United, hivyo kuna kazi kubwa ya kufanya kupenya kwa vigogo hawa.
Sunderland (pointi 19, tofauti ya mabao -22)

Nini kinaendelea?


Kocha wa klabu hiyo, David Moyes, hajataka kuwa mnafiki juu ya hali halisi inayoikumba klabu yake katika miezi michache ya hivi karibuni.

Amekuwa akikiri kabisa kwamba hali ni mbaya, tofauti na wengi wanavyosubiri kwamba atatoa kauli ya kuwatia moyo wachezaji wake katika kipindi hiki kigumu.

Katika dirisha dogo la usajili Januari, alinyakua wachezaji wake wa zamani aliowanoa pale Everton na angalau wakampa ushindi wa bao 4-0 dhidi ya Crystal.

Hakuna aliyewahi kufikiri kuwa Sunderland ingetoa kichapo cha namna hiyo, ikizingatiwa hawakushinda mechi saba hapo awali na mechi iliyofuata, wakabamizwa 4-0 na Southampton.

Unapiga nne, unapigwa nne, ni kama umejitoa mhanga kuweka dau la mke kwa jiwe!

Wana sababu ya kuwa na matumaini?

Zipo mbili:


(i) Mshambuliaji wao, Jermain Defoe.

(i) Mabao yake 14 ya Ligi Kuu England hadi sasa akiwa na umri wa miaka 34 ni kitu cha kuangaliwa kwa makini mno.

Wana sababu ya kuwa na mashaka?

Misimu ya nyuma waliwahi kuepuka janga la kushuka daraja, lakini msimu huu unaonekana kuwa mgumu zaidi kwao.

Ratiba yao iko vipi?

Mechi ngumu kwao ni dhidi ya Everton, Man City, United, Arsenal na Chelsea.

Katika wiki zao mbili kati ya tatu za mwisho, wana mechi dhidi ya Hull na Swansea, angalau hapa watapumua.
Tathimini ya vita ya kushuka daraja Ligi Kuu ya Uingereza [EPL] Tathimini ya vita ya kushuka daraja Ligi Kuu ya Uingereza [EPL] Reviewed by Zero Degree on 2/15/2017 03:10:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.