Loading...

Vincent Bossou amletea 'Dida' zawadi hii toka AFCON

BEKI wa Yanga, Mtogo Vicent Bossou ambaye alirejea juzi kutoka nchini kwao, amempa kipa wa timu hiyo, Deogratius Munish ‘Dida’ zawadi ya glovu za kudakia zilizotumiwa kwenye fainali za mwaka huu za Kombe la Mataifa Afrika nchini Gabon.

Glovu hizo zilitumiwa na kipa wa timu ya Taifa ya Bossou ya Togo, Kossi Agassa, katika fainali hizo ambapo timu hiyo iliishia hatua ya makundi na kuishuhudia Cameroon ikitwaa ubingwa baada ya kuichapa Misri mabao 2-1 katika mchezo wa fainali.

Bossou ambaye alikuwamo kwenye kikosi cha Togo kwenye fainali hizo za Afcon 2017, alianza mazoezi mepesi na wenzake juzi baada ya kumaliza mapumziko aliyopewa.

Kwenye mazoezi yaliyofanyika juzi na jana jioni, benchi la ufundi la Yanga lilionekana kumpa Bossou mazoezi mepesi, kwani alikosekana kwa zaidi ya wiki mbili kikosini.

Baada ya kumalizika mazoezi ya juzi, Bossou alimwita Dida na kumpa zawadi hiyo ya glovu, akimtaka nyanda huyo kuzitendea haki kwa kutofungwa mabao akiwa langoni.

“Umeziona hizi glovu? Zimetoka mbali sana, zimeombewa kila sehemu zilizokopita, zitunzie heshima yake kwa kuacha kufungwa mabao mepesi,” alisema Bossou akimpasha Dida.

Baada ya kumpa maneno hayo, kipa huyo alizichukua glovu hizo na kumshukuru beki wake huyo na kumwahidi kutoruhusu nyavu zake kutikiswa kirahisi.

“Ahsante kwa zawadi hii nzuri, yaani umezidi kunipa mzuka…umeniletea glovu zilizochezewa kwenye michuano ya Afrika, sasa hapa ni kazi tu,” alitamba Dida.

Kikosi cha Yanga kinatarajiwa kuondoka leo kuelekea Visiwa vya Comoro kucheza mchezo wake wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Ngaya de Mbe, mchezo huo ukiwa umepangwa kupigwa kesho.
Vincent Bossou amletea 'Dida' zawadi hii toka AFCON Vincent Bossou amletea 'Dida' zawadi hii toka AFCON Reviewed by Zero Degree on 2/11/2017 04:26:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.