Loading...

Jinsi jina la Makonda lilivyobamba mitandaoni wiki nzima

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda
Mjadala mkubwa umeibuka kutokana na ukimya na kutoonekana kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda tangu aliposali katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT)- Kimara Jumapili iliyopita.

Makonda, ambaye amekuwa gumzo kutokana na kutakiwa kuonyesha vyeti vyake vya elimu, amekuwa akiandamwa na Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima anayetumia ibada za kila Jumapili kumtaka mkuu huyo wa mkoa aonyeshe vyeti vyake.

Tuhuma za Makonda kughushi vyeti ziliibuka baada ya kuwataja baadhi ya wafanyabiashara, wasanii na viongozi wa kisiasa na dini akiwamo Askofu Gwajima kwenye orodha ya watu 65 aliodai ama wana taarifa au wanahusika na bishara ya dawa za kulevya.

Hata hivyo, licha ya mjadala wa vyeti kuwa mkubwa, Makonda mwenyewe ameshindwa kujitokeza kulitolea ufafanuzi suala hilo, huku Jumapili iliyopita akionekana akizungumza na baadaye kutoa machozi katika Ibada ya KKKT-Kimara.

Mchana wa siku hiyo, Makonda alikwenda kusali katika Kanisa la Living Water lililopo Kawe, lakini jambo lililozua mjadala zaidi ni jioni yake aliposhindwa kujitokeza Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam kumpokea Rais John Magufuli ambaye alikuwa akitokea Mtwara alikofanya ziara ya siku nne katika mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara.

Baadaye ilifahamika kuwa nafasi ya mkuu wa mkoa ilikuwa inakaimiwa na Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Hashim Mgandilwa, ambaye ndiye alijitokeza kumpokea Rais.

Baada ya Mgandilwa kuonekana akikaimu nafasi hiyo, siku iliyofuata kwenye mitandao ya kijamii kulijaa habari zinazoeleza kuwa Makonda alikuwa amekwenda Afrika Kusini.

Mitandao hiyo ilikwenda mbali zaidi baada ya kuonyesha video za mtu anayedaiwa kuwa Makonda akiwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Oliver Thambo wa Johannesburg, huku pia mitandao hiyo ikionyesha tiketi ya ndege yenye jina la mkuu huyo wa mkoa.

Hakuna ofisa yeyote wa Serikali aliyekuwa tayari kuelezea alipo Makonda, ambaye si kawaida yake kuwa kimya kwa wiki nzima anapokuwa Dar es Salaam.
Jinsi jina la Makonda lilivyobamba mitandaoni wiki nzima Jinsi jina la Makonda lilivyobamba mitandaoni wiki nzima Reviewed by Zero Degree on 3/11/2017 11:04:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.