Loading...

Rais Magufuli aagiza mkandarasi anyang’anywe hati yake ya kusafiria

Rais John Magufuli ameagiza mwakilishi wa kampuni ya ukandarasi ya Overseas Infranstructure Alliance Private Limited ya India , Rajendra Kumar na wasaidizi wake wanyang’anywe hati za kusafiria hadi watakapomaliza ujenzi wa mradi wa maji wa Ng’apa mjini Lindi.

Rais ametoa agizo hilo leo alipotembelea mradi huo unaotarajiwa kuzalisha zaidi ya lita za ujazo milioni 5 za maji kwa siku kwa ajili ya wakazi wa Mji wa Lindi.

Ameonya kuwa endapo mradi huo hautakamilika katika kipindi cha miezi 4 kuanzia sasa atachukua hatua dhidi ya wanaopaswa kuusimamia.

"Ikipita miezi minne nisilaumiwe, hatuwezi kukubali wananchi wa Lindi wanashida ya maji, fedha zimetolewa, mkandarasi anaamua kupeleka fedha India, mradi umecheleweshwa kwa miaka miwili na mkandarasi hayupo kwenye eneo la ujenzi halafu mnaopaswa kumsimamia mnamuangalia tu wakati sheria zipo, kwa nini hamkumfukuza muda wote huu?" amehoji Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesikitishwa na usimamizi mbaya wa mradi huo ambao tayari kiasi cha Shilingi bilioni 21.8 zimetolewa kati ya Shilingi bilioni 29 zilizopangwa kutumika hadi utakapokamilika.

Waziri wa Maji na Umwagiliaji Gerson Lwenge amesema mradi huo unatekelezwa kwa mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW) na Jumuiya ya Ulaya (EU).

Ujenzi wa mradi huo uliojengwa kwa asilimia 85 hadi sasa ulipangwa kukamilika Machi 17, mwaka 2015.
Rais Magufuli aagiza mkandarasi anyang’anywe hati yake ya kusafiria Rais Magufuli aagiza mkandarasi anyang’anywe hati yake ya kusafiria Reviewed by Zero Degree on 3/04/2017 12:10:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.