Loading...

TEF yaipongeza Clouds kwa jambo hili

BODI ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) imekipongeza Kituo cha Clouds kwa kumsimamisha kazi mtangazaji aliyekiuka msimamo wa kutotangaza habari za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Theophil Makunga, alisema hayo jana katika taarifa yake aliyoituma kwa vyombo vya habari Dar es Salaam.

“Tunawasisitiza wahariri wa vyombo vya habari, magazeti, redio na televisheni kuendelea na msimamo wa kususia habari za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam hadi atakapotimiza matakwa ya kuomba radhi kwa tukio la kuvamia kituo cha Clouds,” alisema.

Alisema TEF imewasiliana na uongozi wa Umoja wa Klabu ya Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na kukubaliana kwamba msimamo huo uendelee.

“Bodi imekutana leo (jana) Dar es Salaam, pamoja na mambo mengine imejadili mwenendo wa vyombo vya habari ndani ya wiki moja tangu tulipotoa msimamo wa kutotangaza habari zake,” alisema.

Makunga alisema bodi hiyo imepitia habari za mkuu huyo wa mkoa zilizochapishwa tangu ulipotolewa msimamo wa kumfungia.

“Bodi inapenda kawapongeza wahariri wote waliotekeleza kwa usahihi msimamo wa kutochapisha habari za mkuu wa mkoa kwa wiki nzima,” alisema.

Alisema Bodi hiyo inatoa wito kwa viongozi wa mitandao ya jamii kuunga mkono msimamo huo.

“Mkuu huyo wa Mkoa amewekewa vikwazo maalum (Smart Sanction) kwa mikutano atakayoiandaa au matukio atakayoyaongoza habari zake hatutazichapisha,”alisema Makunga.
TEF yaipongeza Clouds kwa jambo hili TEF yaipongeza Clouds kwa jambo hili Reviewed by Zero Degree on 3/31/2017 11:00:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.