Loading...

TFF yaizuia klabu ya Yanga kuhama Dar

UONGOZI wa Yanga umefuta safari ya timu yao kisiwani Pemba kutokana na kubanwa na ratiba ya Ligi Kuu Tanzania Bara na Kombe la FA.

Yanga ilipanga kutimkia Pemba kwa ajili ya maandalizi ya mechi yao ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Zanaco ya Zambia, utakaopigwa Machi 11 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katibu Mkuu wa Yanga, Boniface Mkwasa, alisema timu hiyo haitasafiri tena Pemba badala yake itaendelea na maandalizi yake jijini Dar es Salaam.

Alisema ofisi yake iliandika barua kwa Bodi ya Ligi Kuu ikiomba mechi zao zisogezwe mbele ikiwamo ya kesho ya ligi kuu dhidi ya Mtibwa Sugar na ile ya FA, kati yao na Kiluvya itakayofanyika Jumanne ijayo lakini maombi yao yaligonga mwamba.

“Huwezi kwenda Pemba Jumatano halafu ukarudi Ijumaa, hivyo hatutaondoka tutaweka kambi hapa hapa Dar es Salaam, japo hatukutaka iwe hivyo, kwa kuwa wakubwa wameamua tufafanya hivyo,” alisema Mkwasa.

Hata hivyo, alisema wataitumia mechi ya kesho na ile ya Jumamosi kama maandalizi ya mechi dhidi ya Zanaco.

“Tuna mtihani mkubwa mbele yetu, tunataka kutetea ubingwa wetu, tunataka kufanya vizuri katika michuano ya kimataifa, tutahakikisha tunafanya vizuri michezo yote,” alisema Mkwasa.

Yanga itavaana na Zanaco baada ya kuitoa Ngaya FC ya Comoro kwa jumla ya mabao 6-2, ikishinda mabao 5-1 ugenini kisha kutoka sare ya bao 1-1 nyumbani kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
TFF yaizuia klabu ya Yanga kuhama Dar TFF yaizuia klabu ya Yanga kuhama Dar Reviewed by Zero Degree on 3/04/2017 12:17:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.