Loading...

Niyonzima alivyorejesha amani ndani ya Yanga

KIUNGO fundi wa Yanga, Mnyarwanda Haruna Niyonzima, amerejesha amani ndani ya klabu hiyo kutokana na kiwango alichokionyesha mwishoni mwa wiki dhidi ya Prisons ya Mbeya na hivyo kuwapa matumaini makubwa wapenzi wao juu ya matarajio yao ya taji la Ligi Kuu Tanzania Bara kubaki Jangwani.

Sambamba na kiwango hicho, pia mkali huyo amefunguka maneno mazito juu ya mapenzi yake na Yanga na jinsi asivyo tayari kuondoka Jangwani.

Niyonzima alisema bado wana nafasi kubwa ya kutetea ubingwa wao iwapo wachezaji wote ndani ya kikosi hicho wataungana na kuwa kitu kimoja na kuwataka wachezaji wenzake kusahau matatizo yaliyompata kiongozi wao.

“Matatizo yapo, lakini kwanza tushinde, kisha ndio tuwe na nguvu ya kudai kitu na tukishinda ubingwa hata mabosi watakuwa na furaha na kutujali sisi wachezaji,” alisema Niyonzima.

Niyonzima alisema kwa kufanya hivyo wana uhakika mkubwa wa kuchukua ubingwa msimu huu licha ya kukabiliwa na upinzani mkali katika michezo yao minne waliyobakisha dhidi ya Kagera Sugar, Mbeya City, Mbao FC na Toto Africans ya Mwanza.

Katika hatua nyingine, Niyonzima amewashukuru mashabiki na wapenzi wa timu hiyo kwa kuendelea kuwapa sapoti, huku akisisitiza yupo tayari kuongeza mkataba mpya na Wanajangwani hao kutokana na mafanikio makubwa aliyoyapata tangu ajiunge nao.

“Hapa ni nyumbani tofauti na Rwanda, nimezoea maisha ya hapa, sina popote pa kwenda, kila kitu katika maisha yangu hivi sasa vinategemea Tanzania… Watanzania ni watu wakarimu sana, lakini pia nashukuru nimeweza kuishi nao vizuri na kunisaidia pale ninapokwama,” alisema Niyonzima.

Alisema akiwa na Yanga, ameweza kuishi nao vizuri na kama mambo yatakwenda sawa, amepanga kustaafu soka lake akiwa na Yanga kwani ndiyo timu iliyompa heshima kubwa ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, winga nyota wa timu hiyo, Simon Msuva, alisema wamekula kiapo kuwa njia pekee ya kumfurahisha kiongozi wao ni kushinda mechi zote nne zilizobaki na kutetea ubingwa wao wa Bara.

Msuva alisema wanatambua kuwa kiongozi wao huyo amepatwa na matatizo, hivyo njia pekee ya kumfariji ni kuhakikisha wanatetea ubingwa wao, akiwataka wachezaji wenzake kuwa na umoja katika kuiletea ushindi timu yao.

“Tunadai mishahara lakini hilo haliwezi kutufanya tushindwe kutimiza majukumu yetu, tunajua bosi wetu alipata matatizo, hivyo njia pekee ya kumfariji ni kushinda kila mchezo ili tuweze kutetea ubingwa wetu,” alisema Msuva.

Kwa upande wake, straika Amis Tambwe, alisema: “Mechi nne zilizobaki ni ngumu, hapa lazima tule kiapo kwa maana umoja na mshikamano ndio silaha yetu, tusahau matatizo ya kutolipwa mishahara, tuchukue kwanza ubingwa ndio tuanze mambo mengine,” alisema Tambwe.

Katika mbio za ubingwa, Yanga wanaonekana kuwa katika nafasi nzuri kwani japo wapo nafasi ya pili nyuma ya vinara Simba wenye pointi 62 kutokana na michezo 28, wao wana michezo miwili mkononi na iwapo watashinda yote, watakuwa wakiongoza ligi kwa tofauti ya pointi tatu dhidi ya watani wao hao wa jadi.
Niyonzima alivyorejesha amani ndani ya Yanga Niyonzima alivyorejesha amani ndani ya Yanga Reviewed by Zero Degree on 5/09/2017 10:50:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.