Loading...

Mdee, Bulaya kulipwa nusu mshahara kwa miezi 10


Wabunge wa Chadema, Halima Mdee (Kawe) na Ester Bulaya (Bunda Mjini) ambao wamesimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge, watalipwa nusu mshahara na posho zinazoambatana nao kwa miezi kumi.

Stahiki hizo ni kwa mujibu wa kanuni ya 75 ya Bunge inayosema, “mbunge aliyesimamishwa hataingia tena sehemu yoyote ya ukumbi na maeneo ya Bunge kwa muda wote atakapokuwa amesimamishwa na atalipwa nusu mshahara na nusu posho zinazoambatana na mshahara huo.”

Vilevile, kutokana na uamuzi huo wabunge hao watakosa siku 65 za Bunge zinazojumuisha siku 25 zilizobaki za Bunge la bajeti linaloendelea, Bunge la Oktoba na lile la Februari, 2018. Vikao vya mabunge hayo mawili; la Oktoba na Februari kila kimoja huwa na mikutano ya wiki mbili mbili.

Wabunge hao walisimamishwa juzi kwa azimio la Bunge licha ya kutokuwapo au kujitetea kutokana na tuhuma zilizokuwa zinawakabili za kudharau kiti cha spika.

“Tukutane Bunge lijalo la bajeti,” alisema juzi Spika wa Bunge, Job Ndugai. Bunge la bajeti huanza mwezi Aprili.

Kufikia uamuzi huo, kamati ya haki, maadili na madaraka ya Bunge ilisema iliwatafuta kwa simu wabunge hao, lakini haikuwapata. Pia, iliwatumia ujumbe mfupi ambao haukujibiwa na ilipowapelekea hati ya wito haikuwakuta majumbani kwao.

Kwa kutambua umuhimu wa agizo ililonalo na kuzingatia matakwa ya kisheria, hati hizo ziliachwa baada ya kuelezwa kwamba wahusika hawapo kwani wamesafiri. Baada ya jitihada hizo kushindwa kuzaa matunda, kamati iliendelea kuwajadili bila wao kuwapo na kutoa maazimio hayo.

Spika kuburuzwa Mahakamani:

IKIWA ni siku chache baada ya Spika Job Ndugai kuwasimamisha wasihudhurie Bunge hadi mwakani, mbunge wa Kawe, Halima Mdee na Ester Bulaya wa Bunda Mjini wote wa Chadema wamefunguka ya moyoni na kumtolea uvivu spika huyo kwamba asidhani yupo juu ya sheria huku wakiahidi kutinga mahakamani kuidai haki yao.

Wakiwa mkoani Kilimanjaro kwenye mazishi ya mzee Philemon Ndesamburo, wabunge hao walipata fursa ya kuzungumza na waandishi wa habari kuhusiana na adhabu hiyo, na hiki ndicho walichokisema.

Kwa upande wa Ester Bulaya, alidai Ndugai amekuwa kiongozi wa uvunjifu wa amani bungeni akifuatiwa na wafuasi wengine wa CCM, lengo lao likiwa ni kuwanyamazisha wapinzani. Akakumbushia tukio la spika huyo kumpiga mpinzani wake wakati wa harakati za kura za maoni na kumuelezea kwamba ni mtu asiyeweza kudhibiti hasira na ambaye viatu vya ubunge havimtoshi.

Bulaya alisema yeye ndiye aliyewashawishi wenzake wagome na kutoka bungeni lakini alifanya hivyio kama kiongozi kuwalinda wabunge wake wasiendelee kutukanwa na kudhalilishwa na wafuasi wa CCM.

Kwa upande wa Halima Mdee, yeye alisema Ndugai na wabunge wa CCM lazima waelewe kwamba bunge linaongozwa kwa sheria na kwa sababu hii si mara ya kwanza wao kusimamishwa, watakwenda mahakamani kuhakikisha haki inapatikana.

Mdee aliongeza kuwa Ndugai anajua kwamba alifanya makosa ndiyo maana anaogopa wao wasiende mahakamani lakini lazima watafute haki mahakamani. Akazungumzia suala la polisi wa bunge kuondolewa bungeni kwa kushindwa kumshughulikia Mnyika kisawasawa kuwa ni dalili ya hatari kwa bunge.
Mdee, Bulaya kulipwa nusu mshahara kwa miezi 10 Mdee, Bulaya kulipwa nusu mshahara kwa miezi 10 Reviewed by Zero Degree on 6/07/2017 03:45:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.