Loading...

Akamatwa na pembe za ndovu zenye thamani ya milioni 33


POLISI mkoani Morogoro inawashikilia watu watatu akiwamo aliyekutwa na pembe mbili za ndovu zenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 33. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei (pichani) alisema mtuhumiwa wa pembe za ndovu alikamatwa Juni 29, mwaka huu saa tano asubuhi katika Kata na Tarafa ya Mlali, Wilaya ya Mvomero mkoani hapa.

Kamanda Matei alisema askari Polisi wakiwa doria, walipokea taarifa za kiintelejensia na kumkamata mtuhumiwa Kimosa Kibona (43), mkazi wa Kata ya Mlali na alipopekuliwa alikutwa akiwa na pembe mbili za ndovu alizohifadhi kwenye mfuko wa sandarusi.

Alisema mtuhumiwa huyo anaendelea kuhojiwa na hatua za kumfikisha mahakamani zinatafuata baada ya kukamilisha upelelezi. Katika tukio jingine, mkazi wa Msamvu katika Manispaa ya Morogoro, Sunday Balinos (26) anashikiliwa na Polisi baada ya kukutwa akiwa na kilo moja za dawa zinazodhaniwa kuwa ni za kulevya aina ya heroine alizohifadhi katika mfuko wa rambo wa rangi ya njano.

Kamanda Matei alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa Juni 30, mwaka huu saa mbili usiku katika maeneo ya Msamvu Check Point, Manispaa ya Morogoro, ambako askari wakiwa doria walipokea taarifa za kiitelejensia na kumkamata mtu huyo na anaendelea kuhojiwa ili hatua za kumfikisha mahakamani zichukuliwe.

Mtuhumiwa wa tatu ni Stephano Felician (32) ambaye ni mkazi wa Mbezi, Dar es Salaam anashikiliwa na Polisi baada ya kukutwa na bangi debe moja aliyokuwa amehifadhi kwenye mfuko wa sandarusi uliozungushiwa kwa nje mfuko wa rambo.

Kamanda Matei alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa Julai 2, mwaka huu saa nane mchana akiwa Stendi ya Msamvu na pikipiki mbili tofauti moja ikiwa na namba za usajili T332 BRS SunLG na nyingine isiyokuwa na namba ya usajili. Mtuhumiwa huyo anaendelea kuhojiwa na upelelezi ukikamilika atafikishwa mahakamani kujibu mashitaka yake.
Akamatwa na pembe za ndovu zenye thamani ya milioni 33 Akamatwa na pembe za ndovu zenye thamani ya milioni 33 Reviewed by Zero Degree on 7/05/2017 08:11:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.