Loading...

Wambura apata ulaji FIFA


ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Tanzania (FAT kwa sasa TFF), Michael Wambura, ameteuliwa kuwa kamisaa wa mechi ya kwanza ya kuwania kufuzu kucheza fainali zijazo za Kombe la Dunia kati ya timu ya Taifa ya Uganda (Cranes) na Misri.

Mechi hiyo ya kwanza inatarajiwa kupigwa Agosti 31, mwaka huu kwenye Uwanja wa Namboole jijini Kampala, na timu hizo zitarudiana baada ya wiki moja huko Cairo, Misri.

Akizungumza na Gazeti la Nipashe jana, Wambura, ambaye pia ni mgombea wa nafasi ya Makamu wa Rais katika uchaguzi wa TFF unaotarajiwa kufanyika Jumamosi wiki hii, alisema akiwa kwenye kazi hiyo hutumia vyema nafasi ya kuiwakilisha nchi kwa kufanya kazi kwa uadilifu.

Wambura alisema kuwa Tanzania ina makamisaa wanne tu wanaotambulika kimataifa na kati ya hao wawili ni wanawake na amewashauri wadau wengine kujitokeza kufanya mitihani ili waweze kuongezeka.

"Huu ni uteuzi uliofanywa na Fifa, mara nyingi makamisaa wa hapa nchini huwa tunapata mechi za CAF, nashukuru sasa, pia wakubwa duniani wameanza kutuamini na kutupa nafasi hizi," alisema mwenyekiti huyo wa Chama cha Soka cha Mkoa wa Mara (MARFA). 

Mwezi uliopita Wambura alikuwa kamisaa katika mechi kati ya Zambia na Swaziland ambayo ilikuwa ni ya kusaka tiketi ya kushiriki fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) na pia mchezo mwingine ulikuwa ni kati ya Rayon dhidi ya River United ya Nigeria katika mashindano ya Kombe la Shirikisho.
Wambura apata ulaji FIFA Wambura apata ulaji FIFA Reviewed by Zero Degree on 8/10/2017 12:10:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.