Loading...

Lwandamina: “Mchezaji kukosa penalti ni sehemu ya mchezo”


Kama unakumbuka, juzi Jumamosi mshambuliaji wa Yanga, Mzambia, Obrey Chirwa, alikosa penalti kwa mara nyingine katika mchezo wa kimataifa wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya St Louis ya Shelisheli.

Timu hizo mbili zilipambana katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na Yanga ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Juma Mahadhi.

Hata hivyo, katika mchezo huo, Chirwa alikosa penalti baada ya kupiga shuti nje ya lango ukiwa mpira wa adhabu iliyotolewa na mwamuzi wa mechi hiyo, baada ya Hassan Kessy kufanyiwa faulo na kiungo wa St Louis, Harve Rokotoarison kwenye eneo la hatari.

Kitendo hicho kiliwakera mashabiki wengi wa timu hiyo, huku wakiutaka uongozi wa benchi la ufundi la Yanga linaloongozwa na Mzambia, George Lwandamina kutafuta mpigaji penalti mwingine kwani wamechoshwa na Chirwa ambaye amekuwa akikosa mara kwa mara.

Haya hivyo, maoni hayo ya mashabiki hao wa Yanga, yamepingwa vikali na uongozi wa benchi la ufundi la timu hiyo, chini ya kocha wake mkuu, Mzambia George Lwandamina baada ya kusema kuwa hawana mpango wa kubadilisha mpigaji penalti.

Lwandamina amesema: “Mchezaji kukosa penalti ni sehemu ya mchezo, kwa hiyo sioni sababu ya kuanza kumhukumu Chirwa kwa sababu ya kukosa penalti.

“Ametufungia penalti nyingi sana na muhimu lakini kwa sababu jana (juzi) alikosa penalti ndiyo tumhukumu?” alihoji Lwandamina na kuongeza:

“Haiwezekani kufanya hivyo, jambo kubwa na la msingi tuendelee kuwaunga mkono wachezaji wetu ili waongeze juhudi za kupambana uwanjani ili tuweze kufanya vizuri kwenye mchezo wetu wa marudiano.”

Hata hivyo, alipoulizwa Chirwa kuhusiana na suala hilo, hakutaka kuzungumza chochote.

Yanga itarudiana na St Louis Februari 20, mwaka huu huko nchini Shelisheli na itatakiwa kushinda, kutoka sare au hata kufungwa 2-1, 3-2 na kadhalika ili iweze kusonga mbele katika mchuano hiyo.

Source: Champion
Lwandamina: “Mchezaji kukosa penalti ni sehemu ya mchezo” Lwandamina: “Mchezaji kukosa penalti ni sehemu ya mchezo” Reviewed by Zero Degree on 2/12/2018 03:26:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.