Loading...

Kumbukumbu ya kuzama kwa Meli ya MV Bukoba Mei 21, 1996

Meli ya MV Bukoba ikiwa Ziwa Victoria wakati ilipokuwa ikitoa huduma ya usafirishaji kabla ya kuzama
KIUKWELI tarehe kama ya leo miaka 22 iliyopita haitoweza kusahaulika kirahisi kwenye mioyo ya Watanzania na Ulimwenguni kote, kwani usiku wa kuamkia Mei 21, 1996, meli ya MV Bukoba ikiwa na abiria kati ya 750 na 800 pamoja na wafanyakazi 37 ilizama majini kwenye Ziwa Victoria mwambao wa Bwiru Jijini Mwanza ambapo ilikuwa takribani kilomita 30 kufika nchi kavu.

Ripoti ya Tume ya Jaji Robert Kisanga, iliyochunguza chanzo cha hiyo ilieleza kuwa, kati ya hao, 114 waliokolewa wakiwa hai; wakati 391 waliopolewa wakiwa wamefariki na kuzikwa katika makaburi ya Igoma barabara ya Musoma, nje kidogo ya Jiji la Mwanza. Miili mingine ilichukuliwa na jamaa kuzikwa kwao. Jumla ya miili 332 haikupatikana.

Meli ya Mv Bukoba ikiwa inazama
Kila mwaka, ifikapo Mei 21, viongozi wa dini, wa serikali na wananchi huongozana kwenda eneo la ajali kufanya kumbukumbu.

Hakika Mei 21 Mwaka 1996 Taifa la Tanzania liligubikwa na Msiba Mkubwa ambapo kila mmoja kwa nanma yake aliguswa na Msiba huo ambao uliyagharimu Maisha ya Mamia ya Wapendwa Wetu, baada ya Meli ya MV.Bukoba Kuzama hatua chache kabla ya kutia Nanga Mkoani Mwanza ikitokea
Mkoani Kagera.

Meli ya Mv. Bukoba iliyoundwa mwaka 1979 ikiwa na uwezo wa kubeba mizigo tani 850 na abiria 430 ilizama katika Maji ya Ziwa Victoria Mkoani Mwanza yapata umbali wa kilomita zipatazo 30 kutoka ufukweni mwa maji na kusababisha zaidi ya watu 1,000 kupoteza maisha katika Meli hiyo ambayo tangu kuundwa kwake hadi kuzama kwake ilikuwa na umri wa miaka 17. Jambo la butwaa hapa ni Idadi ya vifo na idadi ya abiria waliookolewa ukilinganisha na Uwezo uwezo wa Meli hiyo wa kubeba abiria 430).

Mnara wa Kumbukumbu ya Kuzama kwa Meli ya MV Bukoba uliopo Makaburi ya marehemu waliotokana na ajali hiyo, Igoma – Mwanza
Pengine tumezoea kuita kwamba Mei 21 Watanzania tunaadhimisha kumbukumbu ya kuzama kwa Meli hiyo ambayo iliigeuza taswira ya Mji wa Mwanza, kwani kwa waliokuwa Mwanza Mwaka huo walipigwa na Butwaa baada ya Uwanja Mkongwe wa Nyamagana ambao mara nyingi hutumika kwa
shughuli za Kimichezo, pale ulipogeuka na ghafla na kutapakaa Maiti za wapendwa wetu, ama hakika inauma sana.

Wakati leo tunakumbuka tukio hili ambalo limeacha simanzi mioyoni mwetu, hebu tujiulize kwa pamoja; Kama ilivyo imani ya watalaamu wa masuala ya usafiri kwamba Usafiri wa Majini ndio usafiri salama kuliko aina nyingine ya usafiri, Je Kwa Tanzania imani hiyo ina mantiki yoyote kwamba vyombo vyetu vya usafiri wa majini ni salama?

Makaburi ya waliokufa kutokana na ajali ya kuzama kwa Meli ya MV Bukoba yaliyopo, Igoma – Mwanza
Lakini wakati tunatafakari suala hilo, pia tukumbuke kujiuliza sisi wenyewe bila kusubiri kusukumwa na mtu hususani wale wenye mamlaka ya kuleta matokeo chanya katika kuboresha hali ya usafiri majini Ikiwemo Mamlaka ya Usafiri wa nchi Kavu na Majini SUMATRA kwamba tulijifunza jambo lolote kutokana na ajali hiyo ya Mv.Bukoba?

Na Kama kuna jambo tulijifunza, je tumefanikiwa kulifanyia kazi ipasavyo jambo hilo? Je kuna hali yoyote ya uwajibikaji (kwa waliopewa dhana ya kusimamia sheria) katika kuzingatia sheria za usafiri na usafirishaji wa majini na nchi kavu? Je, tumekwisha jijengea hali ya kuchukua hatua za uokoaji pale tunapopatwa na majanga ya majini au nchi kavu?

Lakini pia wapo waliohoji na bado wanaendelea kuhoji juu ya taarifa ama ripoti ya uchunguzi wa ajari hiyo ya Mv.Bukoba kama ulifanyiwa kazi ipasavyo? Lakini pia wakiwa bado wanaendelea kujiuliza ni ajari ngapi za vyombo vya majini zimetokea tangu kuzama kwa meli hiyo? Hapo nadhani nawe unazikumbuka ajali kadhaa ambazo tayari zimekwisha kutokea na kuyagharimu maisha ya Watanzania ikiwemo ile ya mv Spice Ireland iliyotokea Septemba 10 mwaka 2011 katika Mkondo wa Nungwi kaskazini Unguja Zanzibar.

Lakini yote Tisa, Kumi ni sintofahamu iliyoibuka juu ya Chanzo cha ajali hiyo mbaya kuwahi kutokea hapa nchini.Wapo waliosema ilikuwa ni Uzembe wa Wakaguzi wa na Waangalizi kwa maana ya Mamlaka husika, Wapo waliosema ilikuwa ni Uzembe wa Nahodha na Timu yake na wapo waliosema chombo kilikuwa kibovu.

Wapo waliodai chombo hicho kilikuwa kimebeba Mizigo na abiria kuzidi uwezo wake na wapo waliodai kuwa abiria wenyewe walisababisha ajali hiyo kwani walilazimisha kupanda Melini ilihali chombo kilikuwa kimejaa huku mlolongo huo ukihitimishwa na wale waliohusisha ajali hiyo na Imani za Kishirikina.

Wapo wengi waliowapoteza ndugu, jamaa na marafiki zao na mmoja wao ambae alimpoteza mpendwa wake katika maisha yake ni Mwanamitindo maarufu hapa nchini ambae pia anafanya shughuli zake barani Ulaya Flavian Matata ambae yeye alimpoteza Mama yake mzazi pamoja na binamu yake.

Flaviana na Balozi Mwanaidi Maajar walishiriki kuweka mashada katika mababuri (Picha zote na Maktaba)
Pamoja na watu wengine, Flaviana Matata amekuwa na desturi ya kukumbuka tukio hilo kwa kufika Mkoani Mwanza katika eneo la Igoma walikohifadhiwa watu waliopeza maisha katika ajali hiyo ya Mv.Bukoba ambapo pia maadhimisho ya kuwakumbuka hufanyika kila mwaka, huku akibainisha kuwa ilimchukua miaka mingi hadi kuamini kuwa ni kweli hayuko na mama yake mzazi, kwa kusema kuwa ni miaka michache iliyopita ndiyo ameweza kuamini kama ni kweli hayuko na mama yake tena.
Kumbukumbu ya kuzama kwa Meli ya MV Bukoba Mei 21, 1996 Kumbukumbu ya kuzama kwa Meli ya MV Bukoba Mei 21, 1996 Reviewed by Zero Degree on 5/21/2018 08:05:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.