Loading...

Breaking News: Maalim Seif afariki dunia



Mwanasiasa mkongwe na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Maalim Seif Sheriff Hamad (76), amefariki dunia.

Akihutubia Taifa kwa njia ya televisheni, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Mwinyi, alisema Maalim Seif alifariki dunia akiwa katika Taasisi ya Magonjwa ya Moyo ya Jakaya Kikwete iliyopo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) alikokuwa amelazwa kwa takribani wiki mbili.

Maalim Seif amefariki dunia akiwa ametumikia wadhifa wa makamu wa kwanza wa rais wa SMZ kwa chini ya siku 100 - akiwa sehemu ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyoundwa baada ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2020.

Kifo chake kinahitimisha safari ya kisiasa ya mwanasiasa mashuhuri kuliko wote wa Zanzibar na kiongozi ambaye alizibeba siasa za upinzani katika visiwa hivyo katika muda wa miaka 30 iliyopita.

Mwezi uliopita, katika hatua isiyo ya kawaida, chama chake cha ACT Wazalendo kilitoa taarifa kwa vyombo vya habari iliyoeleza kwamba Maalim na baadhi ya wasaidizi wake na watu ndani ya familia yake walipata maambukizi ya ugonjwa wa korona.

Hatua hiyo haikuwa ya kawaida nchini Tanzania ambako taarifa kuhusu ugonjwa huo zinatolewa kwa kutumia tafsida na lugha nyingine za picha - na hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa kiongozi maarufu na wa ngazi za juu katika taifa hilo kutangazwa kuwa na ugonjwa huo.

Kifo cha  kimepokelewaje?

Viongozi wa matabaka mbali mbali ndani na nje ya Tanzania wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii kumuomboleeza Maalim Seif Sharif Hamad mara baada ya kifo chake kutangazwa.

Balozi wa Uingereza nchini Tanzania David Concar, amesema amesikitishwa na habari za kifo cha Maalim Seif Sharif Hamad, mwanasiasa mtajika katika siasa za Zanzibar ambaye atakkumbukwa sana. ''Anaacha urithi mkubwa wa huduma, kujitolea na shauku ya kuboresha maisha. Natoa pole kwa familia yake na watu wa Zanzibar.''

Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald J Wright aliandika ''Naungana na Watanzania wote - haswa Wazanzibari - kuomboleza kifo cha cha Maalim Seif. Katika maisha yake ya kisiasa kwa zaidi ya miaka 40, alikuwa mfano wa kiongozi na mtumishi ambaye aliweka maslahi ya watu mbele. Ingawa hatuwezi kuchukua nafasi yake, tunaweza na lazima tuheshimu urithi wake''

Kwa upande wake Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kimeandika katika Twitter yake kuelezea masikitiko yake kufuatia kifo cha Maalim Seif.
Breaking News: Maalim Seif afariki dunia Breaking News: Maalim Seif afariki dunia Reviewed by Zero Degree on 2/17/2021 12:03:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.