Loading...

Amazing Tanzania kuzinduliwa mwezi Mei



DODOMA; Tanzania imepanga kuzindua filamu nyingine ya kutangaza vivutio vya utalii ili kuendelea kutangaza utalii wa Tanzania Bara na Zanzibar.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa bungeni mjini Dodoma, wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2024/205.

Amesema filamu hiyo itakuwa ni ya kipekee baada ya filamu ya Royal Tour ambayo ilileta mafanikio makubwa.

Hatahivyo amesema uzuri wa filamu hii imewashirikisha marais wawili wa Tanzania, akiwemo Rais Dk Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Ali Mwinyi kwa ushirikiano wa pamoja na mwigizaji nguli kutoka nchini China Jing Dong.

“Serikali imetengeneza filamu nyingine yenye hadhi ya kimataifa ya kutangaza utalii ya Amazing Tanzania. Filamu hii imerekodiwa na Mhe. Dk Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania na Mhe. Dk Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mchezaji Filamu nguli kutoka nchini China ajulikanaye kwa jina la Jin Dong.

“Filamu hiyo imeandaliwa kwa lengo la kuvutia watalii hususan kwa soko la China na inatarajiwa kuzinduliwa Mei, 2024,” amesema na kuongeza kuwa kumekuwa na ongezeko kubwa la watalii..

“Mwaka 2023 tumeshuhudia ongezeko la idadi ya watalii wa kimataifa kutoka 1,454,920 mwaka 2022 hadi kufikia watalii 1,808,205 mwaka 2023 sawa na ongezeko la asilimia 8.4.

“Aidha, mapato ya utalii yameongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 2.53 mwaka 2022 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 3.37 mwaka, 2023 sawa na ongezeko la asilimia 33.5,” amesema.

Chanzo: Habari leo
Amazing Tanzania kuzinduliwa mwezi Mei Amazing Tanzania kuzinduliwa mwezi Mei Reviewed by Zero Degree on 4/04/2024 07:59:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.