Loading...

Mgunda apata ushindi wa kwanza


Kaimu kocha mkuu wa Simba, Juma Mgunda amepata ushindi wake wa kwanza kwa mabao 2-0 dhidi ya Mtibwa Sugar katika mchezo wake wa pili wa Ligi Kuu Bara uliochezwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Mgunda alianza kwa sare ya mabao 2-2 akiwa Ruangwa mkoani Lindi mbele ya Namungo katika mchezo wake wa kwanza wa ligi baada ya kubebeshwa majukumu ya kocha Abdelhak Benchikha aliyeachana na timu hiyo.

Mabao ya Simba katika ushindi wa kwanza wa Mgunda yamefungwa na Freddy Michael katika dakika ya 35 na Saleh Karabaka dakika ya 64.

Matokeo hayo yameifanya Simba iliyofikisha pointi 50 kupunguza tofauti ya alama baina yake na Azam yenye 54 ambayo ipo nafasi ya pili kutoka saba hadi nne huku Mnyama akiwa na mchezo mmoja mkononi.


Ndani ya michezo hiyo miwili ambayo Mgunda amekaimu nafasi ya Benchikha yapo mabadiliko kadhaa ambayo yameonekana ikiwemo kupata nafasi kwa baadhi ya wachezaji ambao walikuwa wakisugua benchi.

Miongoni mwa wachezaji hao ni pamoja na Edwin Balua ambaye amekuwa na mchango mkubwa katika matokeo hayo akifunga bao moja dhidi ya Namungo na Karabaka ambaye alifunga katika ushindi wa kwanza wa Mgunda dhidi ya Mtibwa.

Ladack Chasambi ambaye amecheza dhidi ya waajiri wake wa zamani (Mtibwa) naye ni mchezaji mwingine ambaye amepata nafasi katika michezo hiyo ambayo Simba imevuna pointi nne.

Kipigo ambacho Mtibwa Sugar imekumbana nacho mbele ya Simba kinaifanya kuendelea kuwa katika hatari zaidi ya kushuka daraja kutokana na kuendelea kuburuza mkia.

Mtibwa Sugar ipo katika nafasi ya 16 ikiwa na pointi 17 ilizokusanya katika michezo 24 na kwa mwenendo huo inachohitaji ni miujiza kujinasua katika hatari hiyo.

Chanzo: Mwanaspoti
Mgunda apata ushindi wa kwanza Mgunda apata ushindi wa kwanza Reviewed by Zero Degree on 5/03/2024 09:18:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.