Loading...

Elimu BURE kaa la moto Jijini Dar.


Wanafunzi wa darasa la pili wa Shule ya Msingi Mbezi Ndumbwi wakiwa darasani huku wengine wamekaa chini kutokana na upungufu wa madawati shuleni hapo, Dar es Salaam jana.

Dar es Salaam. Wakati Serikali ya Awamu ya Tano ikisisitiza kutoa elimu bure kwa shule za msingi na sekondari, mpango huo umesababisha adha kwa baadhi ya shule ikiwamo kukosekana walimu wa ziada, kuibwa vifaa vya kufundishia na ongezeko la wanafunzi.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika shule za msingi na sekondari katika wilaya za Ilala, Kinondoni na Temeke, umebaini kuwa mpango huo badala ya kuwa msaada kwa walimu umekuwa mzigo unaowapasua kichwa.

Fedha za ruzuku zinazopelekwa katika shule kwa mchanganuo maalumu kulingana na idadi ya wanafunzi, hazikidhi matumizi ya shule hizo hata kwa wiki mbili.

Mchanganuo wa fedha za ruzuku Wilaya ya Kinondoni, unaonyesha kuwa ni shule tano pekee ambazo zimepewa fedha ya chakula ni Kawe A, Mbuyuni, Msasani A, Msewe na Sinza Maalumu, huku nyingine zote zikiwa hazina fedha za kulipa walinzi, bili ya maji, umeme, ukarabati wa madawati, madarasa na vyoo.

Katika Wilaya ya Temeke, shule kadhaa zimevunjiwa madarasa, ofisi za walimu na kuibwa vifaa vya kufundishia, meza, viti kutokana na kukosekana walinzi ambao walikuwa wakilipwa kwa ushirikiano wa shule na wazazi. Mlinzi mmoja hulipwa kati ya Sh150,000 hadi 200,000.

Mpango huo umekuwa mwiba mchungu kwa walimu wa shule hasa za sekondari ambao walitakiwa kuwa wabunifu kwa kutafuta jinsi ya kuongeza ufaulu wa wanafunzi na kushirikiana na wazazi kulipa walimu wa ziada hasa wa masomo ya sayansi.

“Nimeajiri walimu sita wa masomo ya sayansi kwa kushirikiana na wazazi, ambao hapa kwangu nina mahitaji makubwa huku akiwapo mmoja aliyeajiriwa na Serikali. Kwa mwezi nawalipa Sh300,000 hadi 350,000, najiuliza nitawalipa nini na fedha ya ruzuku haina fungu hilo? Bado mlinzi, bado maji, bado umeme, nimechanganyikiwa natamani kurudi kijijini nikalime kuliko fedheha hii, ”alisema mmoja wakuu wa shule ya sekondari wilayani Temeke ambaye hakuwa tayari jina lake liandikwe gazetini.

Alisema mwaka huwa ana mitihani minne wa Machi, Juni, Septemba na Desemba, ambayo kila mmoja hadi unamalizika humgharimu Sh1.5 milioni, kwa bahati mbaya fedha ya ruzuku aliyopata kwa mchanganuo wote ni Sh4.8 milioni hivyo kwa mitihani pekee anatumia Sh6 milioni ambazo hafahamu atazitoa wapi huku fedha za ruzuku zikiacha hayo yote bila majibu wala ufafanuzi.

“...Wazazi wametangaziwa elimu bure kwa kishindo, sielewi itakuwaje na waliendelea kufundisha mwezi uliopita wananidai na sifahamu mwezi huu nitawapa nini,” alisema mwalimu mwingine.

Katika shule za msingi, tatizo kuu lililojitokeza ni wanafunzi kuwa wengi kuliko uwezo wa shule.

“Mwaka jana na mwaka juzi, wiki ya kwanza shuleni nilikuwa nimekadiria kuandikisha wanafunzi 250, wakaongezeka hadi 300, lakini hadi asubuhi ya leo (jana) nimeandikisha wanafunzi 600, ” alisema mwalimu mkuu wa shule moja wilayani Temeke ambaye pia aliomba jina lake lisiandikwe gazetini.

Alisema kwa ongezeko hilo kila darasa watakaa wanafunzi 150 badala ya 50 waliokuwa wanakaa awali.

“Hatuwezi kuwakataa tutaambiwa tunakataa wanafunzi, bado wanakuja hadi Machi, sijui itakuwaje,” alisema mwalimu mwingine wa shule ya msingi wilayani humo.

Alisema mbali ya hilo wamelazimika kutoa elimu ya ziada kwa wazazi, kutokana na wengi wao kuwaleta wanafunzi wakiwa hawana kitu chochote hadi begi la kubebea madaftari.

“Ukiwauliza wazazi mbona mtoto hana kitu zaidi ya sare alizovaa anakuambia wametangaziwa elimu bure, kibaya zaidi hata nembo hawana, tunashindwa kuwaambia walipe Sh500 au 1,000 ya nembo watasema tunawalipisha,” alisema.

Alifafanua ikitokea wanafunzi wamepata matatizo itakuwa ngumu kuwatambua, kutokana na kutokuwa na nembo,” alisema.

Akizungumzia changamoto ya ruzuku, Ofisa Elimu Mkoa wa Dar es Salaam, Raymond Mapunda alisema shule zinazopata tabu ya ruzuku ni zenye wanafunzi wachache kwani zilizo na wengi hazipati adha hiyo kwa kuwa zinapata fedha nyingi.

Alisema Serikali imepanga kila mwanafunzi kwa mwaka atumie Sh10,000 hivyo zitatolewa kidogokidogo hadi zitimie: “Hizo changamoto zilizopo zitafanyiwa kazi taratibu lakini fedha iliyopo itumike kulingana na maelekezo yaliyotolewa.”


Source:Mwananchi
Elimu BURE kaa la moto Jijini Dar. Elimu BURE kaa la moto Jijini Dar. Reviewed by Zero Degree on 1/15/2016 03:08:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.