Loading...

Tanga wamtaka Waziri Lukuvi akatumbue ‘majipu’ Idara ya Ardhi.


Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi, William Lukuvi

Tanga. Diwani wa Kata ya Maweni (CCM), Joseph Colvas (CCM) amemtaka Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi, William Lukuvi kufanya ziara ya kuyatumbua majipu katika idara ya mipango miji ya Halmashauri ya Jiji la Tanga kwa madai kuwa inagombanisha wananchi.

Akizungumza katika mkutano na wakazi wa vijiji vinne vya Kange, Kasera, Kichangani na Saruji jana, Colvas alisema idara hiyo imejaa vishoka ambao hupima viwanja vya watu na kuvigawa kwa wengine.

Alisema vishoka hao wamekuwa kero, kwani wananchi sasa hawafanyi kazi za kujiletea maendeleo na badala yake wanashinda kupanga foleni katika ofisi za mipangomiji kwa ajili ya kutaka kujua uhalali wa viwanja vyao.

“Vijiji vyetu vimekuwa vikiingia katika mgogoro usio wa lazima na hii inatokana na idara yetu yenye dhamana kuwalea vishoka, tunamuomba waziri mwenye dhamama aje kuyatumbua majipu haya,” alisema Colvas na kuongeza:

“Nawaomba ndugu zangu wananchi tuwe watulivu, tusigombane wenyewe kwa wenyewe, tunajua pale mipangomiji kuna majipu yanataka kutumbuliwa na karibuni kazi hiyo itafanyika.” Kwa upande wake mjumbe wa kamati ya mgogoro wa viwanja vya Kange, Suleiman Bindo, alisema kuna mapapa wanaowauzia matajiri viwanja vya wanyonge na kuitaka Serikali kuwashughulikia.

Alisema kuna kesi nyingine mahakamani zinazohusiana na migogoro ya ardhi katika jiji hilo.

“Viwanja vyetu vinaporwa kwa vile hatuna uwezo wa kwenda ngazi za juu kulalamika, tumechoka kunyanyaswa,” alisema.


Source: Mwananchi
Tanga wamtaka Waziri Lukuvi akatumbue ‘majipu’ Idara ya Ardhi. Tanga wamtaka Waziri Lukuvi akatumbue ‘majipu’ Idara ya Ardhi. Reviewed by Zero Degree on 1/12/2016 11:16:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.