Loading...

Wapigwa marufuku kuuza pombe saa za kazi.


Mvomero. Wafanyabiashara wa pombe za kienyeji wa Kijiji cha Bunduki wilayani Mvomero, wametakiwa kuacha kuuza pombe saa za kazi.

Imeelezwa kuwa hali hiyo inachangia watu wengi kuacha kufanya kazi za maendeleo na kushinda vilabuni kutoka asubuhi hadi jioni.

Diwani wa Kata ya Mvomelo, Prosper Mkunule alitoa kauli hiyo juzi alipokuwa akizungumza na wakazi wa Kata ya Bunduki.

Alisema uzalishaji na shughuli mbalimbali za maendeleo kijijini hapo umeshuka kwa sababu ya unywaji pombe kupita kiasi.

Alisema: “Kwanza uuzaji wa wakati wa muda wa kazi ni ukiukwaji wa sheria ndogo ndogo walizojiwekea kwenye kata hiyo. Yeyote atakaye kiuka sheria hii atafungiwa kibanda chake cha biashara na atachukuliwa hatua zaidi.”

Aliwataka wakazi wa kijiji hicho kuacha tabia ya unywaji wa pombe hovyo na badala yake wajikite katika shughuli za kuwaingizia kipato.

Mkazi wa eneo hilo, Prakseda John alisema kijiji hicho kimekumbwa na upungufu mkubwa wa chakula uliochangiwa na watu kushindwa kujishughulisha na kilimo na badala yake kushinda kwenye pombe.

Alisema Taifa linapotenza nguvu kazi kwani vijana wengi wanaotegemewa wawe wazalishaji wakubwa, wanashinda kwenye pombe.

Mkazi mwingine, Monica Alex alisema miaka ya nyuma kijiji hicho kilikuwa kimbilio la vijiji jirani kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya chakula yakiwamo mahindi, ndizi na mbogamboga.

Alisema kama viongozi watasimamia sheria ndogo iliyotungwa kuhusiana na unywaji wa pombe muda wa kazi, itasaidia kuwafanya watu wafanye kazi ya kilimo kama zamani.


Source: Mwananchi
Wapigwa marufuku kuuza pombe saa za kazi. Wapigwa marufuku kuuza pombe saa za kazi. Reviewed by Zero Degree on 1/12/2016 01:55:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.