Loading...

Hizi hapa GHARAMA za kuingia bungeni kupitia jimbo lolote kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi.


Sh33 mil - 88mil: Fedha ambazo wagombea ubunge wanatakiwa kutumia kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi.

Dar es Salaam. Ukitaka kuingia bungeni kupitia jimbo lolote nchini, andaa mamilioni ya shilingi na katika baadhi ya maeneo yanafikia hata Sh1 bilioni.

Kumekuwa na matamanio miongoni mwa wananchi kutaka kuingia katika siasa na hasa kuwa wabunge, lakini fedha zimekuwa kikwazo cha kufanikisha ndoto hiyo.

Utafiti uliofanywa na gazeti hili kwa kuwahusisha baadhi ya wabunge wa mihula mbalimbali, umebainisha kwamba hakuna namna, kila mtia nia ni lazima azame zaidi mfukoni ili kutimiza ndoto yake.

Agosti 18 mwaka jana, Serikali ilitoa waraka unaotokana na Sheria ya Gharama za Uchaguzi unaokitaka kila chama cha siasa kutumia kiwango kisichozidi Sh17 bilioni katika kampeni zake za uchaguzi wa Rais.

Waraka huo ulikuwa kwenye Tangazo la Serikali Namba 325 lililokuwa na kichwa “Amri ya Gharama za Uchaguzi Mwaka 2015” lililosainiwa na aliyekuwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Sheria hiyo ilionya: “Fedha za ziada ambazo zinaweza kutumiwa katika mazingira maalumu kama gharama za uchaguzi, hazitatakiwa kuzidi asilimia 15 ya gharama ya kiasi halisi cha fedha kilichoanishwa katika jedwali.”

Akizungumzia gharama hizo, mkuu wa kitengo cha mawasiliano katika Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Monica Lawrence alisema kwa mujibu wa sheria hiyo, ndani ya siku 180 ofisi hiyo inaendelea kupokea ripoti za vyama vya siasa kuhusu matumizi ya gharama za uchaguzi.

Ingawa sheria hiyo inabainisha kuwa mgombea ubunge anatakiwa atumie kati ya Sh33 milioni hadi Sh88 milioni kwa kuzingatia ukubwa wa jimbo, idadi ya watu na miundombinu ya mawasiliano ndani ya jimbo la uchaguzi, wahusika wanasema mara nyingi, huwa zinazidi.

Aliyekuwa mbunge wa Nachingwea (CCM) na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe alisema mambo mengi yamebadilika na thamani ya fedha pia imeshuka jambo ambalo linaathiri kila kitu.

“Sasa hivi ni kawaida kusikia mtu ametumia Sh1 bilioni. Hawa ni wale wanaoutaka ubunge kwa lazima. Wanahonga na kucheza faulo nyingi,” alisema Chikawe ambaye hivi karibuni aliteuliwa kuwa balozi.

Waziri huyo wa zamani wa utawala bora alisema, “zamani walimu walikuwa na uwezo wa kujitokeza na kukidhi vigezo (vya ubunge) lakini sasa tunashuhudia wafanyabiashara ndiyo wanaoweza kuendesha mchakato mzima.”

Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Peter Msigwa alisema licha ya matakwa ya sheria, mfumo wa chama na falsafa za mgombea binafsi, zina mchango kwenye kuongeza au kupunguza gharama hizo.

“CCM ni tofauti na vyama vya upinzani. Ndani ya CCM huwezi kuwa mbunge kama huna Sh600 milioni mpaka Sh1 bilioni. Nilitumia chini ya Sh30 milioni mwaka 2010 na mwaka huu kiasi hicho kimeongezeka kidogo, nimetumia Sh40 milioni. Bado ni ndani ya kiasi kinachoagizwa na Tume ya Uchaguzi,” alisema Mchungaji Msigwa.

Gharama zinazoelezwa kuwa ni muhimu kwa kila mgombea ni zile za kuchukulia fomu, kuandaa mikutano ya kampeni, kukodisha spika, kulipa mawakala, usafiri wa mgombea na wapambe wake, vipeperushi, fulana, kofia, mabango ya matangazo, chakula na vinywaji kwa timu ya kampeni na posho mbalimbali.

Kutoka Zanzibar, Dk Abdulla Saadalla (CCM) alisema gharama huwa zinatofautiana kati ya mgombea anayejitokeza kwa mara ya kwanza na anayeendelea na kusisitiza kuwa kwa wastani ni lazima atumie Sh100 milioni.

“Majimbo ya huku ni madogo na yana wananchi wachache. Kwa mgombea anayejipendekeza sana kwa kushiriki matukio ya kijamii kama ujenzi wa shule, mchango wa vitabu shuleni, jezi za michezo gharama zake zinaweza kuwa kati ya Sh150 milioni mpaka Sh180 milioni.

 Watu huanza mipango mapema kwa kujisogeza kwa wapigakura wao kwa kuchangia mambo mbalimbali,” alisema Dk Saadalla, naibu waziri wa zamani wa iliyokuwa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Aliyekuwa mbunge wa Wete, Mbarouk Salim Ali (CUF) alisema pamoja na kwamba gharama za awali hutolewa na kamati ya utendaji ya chama husika kabla mgombea kujinadi, kwa majimbo madogo kama ya Zanzibar, mtu anahitaji Sh60 milioni ili kukamilisha ndoto yake.”

Ukiacha vigezo vya kisheria, Mahadhi Juma Maalim, aliyekuwa mbunge wa Muyuni (CCM) alisema udhaifu wa mpinzani ni kigezo muhimu cha kushinda.

“Wapo wanaotumia Sh20 milioni lakini wengine hufikisha zaidi ya Sh200 milioni na hii inatokana na ukubwa wa jimbo na kufahamika kwa mgombea.”

Aliyekuwa mbunge wa Karatu (Chadema), Israel Natse alisema kama lengo la mgombea ni kuwatumikia wananchi, hakuna gharama kubwa atakazokutana nazo.

“Usipotoa rushwa huwezi kumaliza Sh50 milioni zinazoelekezwa na Tume. Mimi nilitumia Sh20 milioni na sikutoa rushwa ya aina yoyote. Wananchi wengi walijitoa na kunichangia. Hivi sasa wengi wanapenda ubunge si kwa ajili ya kuwatumikia wananchi, bali sifa ya kinga ya kidiplomasia,” alisema.

Aliyekuwa mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila alisema kuna mambo mawili ya msingi kabla mtu yeyote hajaingia bungeni; mtaji wa rasilimali watu na ule wa fedha.

“Mwaka 2010 nilitumia Sh7 milioni kutoka mfukoni mwangu. Gharama nyingine wananchi walinisaidia. Walinipa magari na mafuta pia, walinisaidia vipeperushi na fulana. Gharama ziliongezeka mwaka jana. 
Nilitumia Sh60 milioni baada ya wadhamini wangu kuamini kuwa ninaweza kulipia mwenyewe. Pamoja na haya yote, watu ndiyo kila kitu ili kufanikisha safari hii,” alisema. 

Gharama hizi hazipo kwa wagombea wa majimboni, viti maalumu pia wanahusika. Dk Sadalla alisema wagombea wa aina hii hutumia zaidi ya theluthi moja ya kiasi cha mgombea wa jimbo.

Hata hivyo, aliyekuwa mbunge wa viti maalumu kutoka Iringa (CCM), Dk Pindi Chana alisema: “Sheria na Katiba ya nchi imependekeza, ipo idadi maalumu ya wanawake wanaotakiwa kwenye nafasi ya uongozi. Wakati nagombea mwaka 2010 nilikuwa mwajiriwa wa halmashauri, nikiwa mwanasheria wa Iringa. Sikuwa na pesa yoyote ya maana. Nilifanya kampeni kwa kupanda daladala na nikafanikiwa.”

Alisema hata chakula alikuwa anapata kutoka nyumbani kwake hivyo kuwatia moyo wanawake wenzake kujitokeza na kutoogopa gharama akisema si za kutisha.

Mbunge wa viti maalumu (Chadema), Suzan Lyimo alisema hakuna gharama kubwa kwa wagombea wa nafasi hizo na kwamba kiwango kimewekwa ambacho si lazima kitumike.

“Sheria inataka tusizidishe Sh11 milioni. Hizo ni fedha nyingi.”

Aliyekuwa mbunge wa Arumeru Magharibi (CCM), Goodluck Ole-Medeye alitahadharisha juu ya rushwa akisema ndiyo inayofanya gharama za uchaguzi kuwa kubwa kuliko kawaida.

“Mimi sihongi wapigakura ila nalipia vipeperushi, kamati ya kampeni yenye wajumbe 20 pamoja na wasaidizi wangu. Ukijumlisha na mambo mengine gharama yake inaweza kuwa Sh60 milioni. Kwa watoa rushwa, inaweza ikazidi Sh100 milioni,” alisema Ole-Medeye ambaye alikihama chama hicho na kujiunga na Chadema.

Ipo tofauti kwa majimbo yaliyo vijijini na yale ya mijini. Aliyekuwa Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Dk Makongoro Mahanga alisema kama mgombea atafuata ratiba aliyowekewa na chama chake kwa ajili ya kampeni ni lazima atatumia fedha nyingi.

Mbunge huyo wa zamani wa Segerea (CCM) ambaye sasa amejiunga na Chadema, alisema kwa majimbo ya Dar es Salaam, kwa mgombea anayejibana, anaweza akatumia walau Sh50 milioni.

“Hiyo ni kwa yule asiyejitangaza sana kwenye jimbo lake lakini kwa wale wanaotaka kubandika picha zao kila nyumba, kusafirisha wajumbe na mambo mengine fedha hiyo haitoshi. Inaweza kufika Sh300 milioni endapo mgombea atafanya kila kitu na akafuata ratiba ya Tume na chama chake kujinadi kwa wananchi wa jimboni kwake,” alisema Dk Mahanga.




ZeroDegree.
Hizi hapa GHARAMA za kuingia bungeni kupitia jimbo lolote kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi. Hizi hapa GHARAMA za kuingia bungeni kupitia jimbo lolote kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi. Reviewed by Zero Degree on 2/24/2016 06:37:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.