Loading...

‘Mazungumzo yalikosa nia njema’, Maalim Seif.


Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, akizungumza na viongozi wa chama hicho ngazi za wilaya na majimbo ya Unguja katika mkutano uliofanyika Kiembe Samaki, Zanzibar. 

Dar/Zanzibar. Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amesema mazungumzo kati yake na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein hayakufanikiwa kwa sababu palikosekana nia njema miongoni mwa wahusika.

Akizungumza na viongozi wa matawi, majimbo na wilaya wa chama hicho Unguja jana, Maalim Seif alisema mazungumzo hayo yaliyodumu kwa zaidi ya miezi miwili yakiwahusisha baadhi ya watendaji wakuu wa CCM Zanzibar, yalishindwa kupata suluhu kutokana na kukosa “nia ya dhati ya kukwamua hali tete ya mkwamo wa kisiasa nchini.”

“Miongoni mwao hawana nia njema na baadhi yao bado wanaamini kutawala kwa mabavu huku wakikosa kuiheshimu Katiba,” alisema kwa msisitizo Maalim Seif na kuongeza:

“Katika vikao vyote tisa tulivyokutana Ikulu ya Zanzibar ni hilo tu lililokwamisha, maana wengine bado wanaota zama za kutawala kwa mabavu, wanaiweka pembeni Katiba na kuyapindua maamuzi ya haki ya umma ya wananchi.”

Alidai kufutwa kwa maamuzi ya Wazanzibari kupitia Uchaguzi Mkuu kulifanywa kwa baraka za baadhi ya waliokuwa watendaji wakuu wa Serikali ya Muungano.

Wakati huo huo, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC) kimemtaka Mwenyekiti wa Zec Jecha Salim Jecha kujiuzulu kwa madai ya kukiuka Katiba, Sheria na Kanuni za uchaguzi pamoja na misingi ya demokrasia, utawala wa sheria na utawala bora.

Kaimu Mkurugenzi wa Kituo hicho, Imelda Urio alisema marudio ya uchaguzi huo ni ukiukwaji wa haki za kibinadamu na misingi ya demokrasia na utawala bora kwa sababu Katiba ya Zanzibar na sheria ya uchaguzi hazijampa mamlaka Mwenyekiti au Zec kufuta uchaguzi.

Wakati huo huo, Jaji Mkuu wa Kenya Dk Willy Mutunga ameshauri kuendelea na mazungumzo ya kutafuta suluhu ya kisiasa Zanzibar kwa lengo la kuimarisha Muungano wa Tanzania, huku akionesha hofu kuwa ukivunjika unaweza kuwa na athari kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla.

Jaji Mutunga alitoa ushauri huo jana wakati akizungumza na waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dar es Salaam.

Credits: Mwananchi




ZeroDegree.
‘Mazungumzo yalikosa nia njema’, Maalim Seif. ‘Mazungumzo yalikosa nia njema’, Maalim Seif. Reviewed by Zero Degree on 2/04/2016 11:50:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.