Loading...

Amri ya Rais Magufuli yauma CCM, Ukawa.

AMRI ya Rais, John Magufuli, kukataza mikutano vyama vya siasa nchini mpaka mwaka 2020 kwa viongozi wasiopigiwa kura na wananchi.

Imeng’ata vyama vyote baada ya Msemaji wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Christopher Ole-Sendeka, kufanya mkutano aliouita harambee wilayani Longido, mkoani Arusha, huku akiliambia gazeti hili kwamba ufafanuzi zaidi unahitajika kwa sababu ilani yao inawataka kutembelea utekelezaji wake na miradi ya maendeleo.

Ole Sendeka aliiambia Nipashe jana kwa kuwa, wao ni chama tawala, wana jukumu la kuisimamia serikali hivyo wasifananishwe na wapinzani.

Wakati Ole-Sendeka akiyasema hayo, Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, jana pia aliiambia Nipashe kwamba, kutokana na hali ilivyo sasa, ni vizuri kukawa na mjadala na wadau wa siasa kupitia majukwaa walionayo badala ya kuendelea kujadili mambo hayo kwenye vyombo vya habari.

Haya yametokea wakati viongozi wa vyama vya upinzani wamekuwa wakizuia kufanya mikutano pamoja na kushiriki katika mikutano tofauti ya kisiasa kama mahafali.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa alizuiwa Jumamosi iliyopita kuhudhuria shughuli ya mahafali ya waumini wa Kanisa la Kiinjilisti la Kilutheri Tanzania waliohitimu Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili (MUHAS).

Msimamo wa Magufuli

Akiwa mkoani Singida Julai 29, Rais Magufuli alisisitiza amri aliyoitoa mwishoni mwa Juni mwaka huu ya kupiga marufuku shughuli za kisiasa hadi mwaka 2020, akisema wabunge na madiwani ndio wanaopaswa kufanya mikutano na shughuli nyingine kwenye maeneo yao walimopigiwa kura huku yeye akizunguka nchi nzima kwa sababu ndiyo jimbo lake.

Rais Magufuli alisema: "Wabunge wanaruhusiwa kufanya mikutano kwenye maeneo yao bila kuwa na wasiwasi. Akitaka kufanya mkutano hapa, afanye pale, yule amechaguliwa kwa kazi ile katika jimbo lake. Diwani anaruhusiwa kufanya mikutano yake kwenye eneo lake kuwahamasisha watu walete maendeleo. Na mimi nilichaguliwa urais, jimbo langu ni Tanzania nzima.

“Hakuna Rais mwingine badala ya John Pombe Joseph Magufuli. Kwa hiyo, na mimi nitazungukia majimbo yangu yote, nikawaeleze wananchi ninachotakiwa kukifanya ndani ya miaka mitano."

"Kwa hiyo, kama upo Mbunge wa Chadema, uko kwenye jimbo lako la Hai, zunguka Hai mpaka uchoke. Fanya mikutano kila kijiji, kila kata mpaka jimbo lako likamilike. Kama wewe ni mbunge wa Chadema au wa chama gani sikijui, jimbo lako ni mahali fulani, nenda ukafanye kule kazi,” alisema Rais Magufuli.

KAULI YA OLE-SENDEKA

Wakati Magufuli akisema hayo, jana Ole-Sendeka alikiri kuendesha mkutano aliouita wa harambee uliofanyika wilayani Longido juzi.

"Jana (juzi) kulikuwa na mkutano wa harambee ya kikundi cha kina mama ambao ulifanyika kwenye 'site' (eneo) lao la ujenzi wanakojenga ofisi ya Vicoba ya kwao wenyewe.”

“Si CCM pekee walioshiriki, hata diwani wa Chadema alishiriki. CCM, Chadema, CUF, walishiriki, vyama vyote vilishiriki ila mgeni rasmi nilikuwa mimi," alisema.

Msemaji huyo wa CCM aliongeza kuwa, ipo haja ya kupata ufafanuzi zaidi kuhusu tamko la Rais Magufuli kuzuia mikutano ya kisiasa kwa viongozi wasio wa kuchaguliwa na wananchi kutokana na tamko hilo kukinzana na ilani ya uchaguzi ya chama tawala.

"Lakini nilichozungumza hapa (Longido), nilisema habari ya maandamano hapana. Iwe mikutano ya kisiasa na ya hadhara kama ilivyokuwa wakati wa kampeni hapana.

Rais aliyepewa dhamana na wananchi, anazunguka na wabunge watazunguka. CCM kama chama tawala kina nafasi yake ya kufuatilia utekelezaji wa ilani ya chama chake. Na kwa kufanya hivyo wala huwezi kulinganisha CCM na upinzani. CCM ina dhamana, mkataba wa wananchi waliopiga kura.

“Chama kilichopo madarakani, pale serikali yake inapotekeleza ilani, chama hicho kina jukumu la kusimamia utekelezaji wa ilani. Kwa hiyo, nitazishangaa kamati za siasa za wilaya zisipozunguka kukagua miradi ya maendeleo katika maeneo yake kama ilani yao inatekelezwa.

Sisi (CCM) tuna dhamana ya kuhakikisha huduma zinatolewa na tunatekeleza ilani ya uchaguzi. Kwa hiyo miradi ya maendeleo, kukagua hiki na kile tutakwenda tu.

“Tutapata 'clarity' (ufafanuzi) kama ibara ya mwisho ya ilani ya CCM imewekwa pembeni. Mkataba tulionao na wananchi ni ilani ya uchaguzi ya CCM.

Kwenye ilani ya uchaguzi ya CCM, imeagiza viongozi wa CCM kuhakikisha wanatembelea kupitia vikao vyao vya wajumbe wa kila ngazi kwenda kuona utekelezaji wa ilani, kukagua miradi ya maendeleo katika maeneo yao na kuhamasisha maendeleo. Haya ni mambo ambayo yatahitaji ufafanuzi zaidi baadaye."

JAJI MUTUNGI

Kwa upande wake, Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Mutungi jana alilalamikia kile alichodai ni upotoshwaji wa tamko lake alilolitoa hivi karibuni.

“Tangazo la sajili limetumiwa vibaya kuonyesha umma kwamba huyu msajili si mkweli. Kama mnamtuhumu msajili kuwa ni ‘bias’ (ana upendeleo), lakini mbona hamuelezi kwamba huyuhuyu msajili aliwaambia kama suala hili mmelipeleka mahakamani, maana yake mmemfunga mdomo, hawezi kuliongelea?” alihoji Jaji Mutungi.

“Nilichotegemea sana sana ni kwamba itabidi tukae kwenye kikao. Hili (la kikao) ni suala la sekretarieti, lakini itafika mahali nitawaambia kwanini tukimbilie kwenye 'media' (vyombo vya habari) badala ya kukaa kwenye ‘forum’ (jukwaa) zetu."

Lissu agongelea msumari

Alipotafutwa na waandishi wa habari jana, Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, alisema Ole-Sendeka hajakosea kufanya mkutano licha ya zuio la Rais Magufuli kwa kuwa katiba inamruhusu.

"Mimi sitasema kwamba Ole-Sendeka amekosea, hajakosea kwa sababu ana haki ya kufanya mikutano ya kisiasa mahali popote kwa mujibu wa katiba ya nchi hii, kwa mujibu wa sheria ya vyama vya siasa na kwa mujibu wa sheria za Jeshi la Polisi," alisema Lissu.

Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema) na Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, aliendelea kusema kwamba, "kwa hiyo, suala la kwamba Ole-Sendeka azuiliwe asifanye mikutano si sawasawa. Asizuiliwe kufanya mikutano, na sisi tusizuiliwe kufanya mikutano kwa sababu haki yetu ya kufanya mikutano ni ya kikatiba na kisheria.”

Kauli ya JK

Wakati wa Mkutano Mkuu Maalum wa CCM uliofanyika Julai 23, mwaka huu, Rais mstaafu Jakaya Kikwete, alitofautiana pia na msimamo wa mrithi wake wa kupiga marufuku shughuli za kisiasa pale aliposema, viongozi wa chama hicho, wamekuwa hawaendi kwa wananchi na jambo hilo ndilo linalofanya chama hicho kutumia nguvu nyingi kushinda.

“Viongozi wamekuwa wazito kutoka kwenda kwa wananchi, matokeo yake watani zetu ndiyo wanaokwenda…sijui ni kwa sababu wanasema wao ni chama tawala? Hata kama ni chama tawala, ipo siku utatoka tu kwa sababu huendi kwa wananchi, matokeo yake wakati wa uchaguzi unatumia nguvu kubwa kushinda,” alisema Kikwete kwenye mkutano huo wakati aking’atuka kama Mwenyekiti wa CCM.

Credits: Nipashe(IPPMedia)
ZeroDegree.
Amri ya Rais Magufuli yauma CCM, Ukawa. Amri ya Rais Magufuli yauma CCM, Ukawa. Reviewed by Zero Degree on 8/02/2016 09:20:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.