Loading...

Vifo vyatikisa Bunge.

Waziri mkuu Kasimu Majaliwa, Spika wa Bunge, Job Ndugai na Kiongozi wa Upinzania bungeni, Freeman Mbowe (kulia) wakiangalia mwili wa Mbunge wa Dimani, Hafidh Ally Tahir ukipandishwa kwenye ndege katika uwanja wa ndege wa Dodoma kusafirishwa kwenda Zanzibar kwa maziko jana.
KWA mara ya kwanza katika historia ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bunge hilo liliahirishwa jana bila hotuba ya Waziri Mkuu, badala yake alitoa hoja tu ya kuliahirisha.

Hatua hiyo inatokana na kifo cha ghafla cha Mbunge wa Dimani, Hafidh Ali Tahir (CCM), aliyefariki saa nane usiku wa kuamkia jana wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.

Mbunge Tahir pia amefariki dunia huku Bunge likiwa katika msiba mwingine wa Spika mstaafu Sitta, aliyefariki Novemba 7, mwaka huu nchini Ujerumani. Hii ni mara ya pili kwa Mkutano wa Tano wa Bunge kuahirishwa kutokana na msiba, Novemba 7, mwaka huu liliahirishwa kutokana na kifo cha Spika mstaafu wa Bunge, Samuel Sitta.

Spika wa Bunge, Job Ndugai jana asubuhi alitoa taarifa ya kifo cha Tahir na kusema Bunge lipo katika kipindi kigumu kisichoelezeka. Alisema Bunge limepokea kwa mshituko taarifa hiyo kwa sababu bado walikuwa katika majonzi ya msiba wa Sitta wiki hii na sasa msiba mwingine wa Mbunge.

Kwa mujibu wa Ndugai, juzi alikuwa naye mpaka usiku wakizungumza masuala ya uongozi na michezo na alipopata taarifa asubuhi jana kuwa amefariki, alishtuka sana.

“Kwa masikitiko makubwa, natangaza kifo cha Mbunge mwenzetu wa Dimani, Zanzibar, mheshimiwa Hafidh Ali Tahir kilichotokea ghafla usiku saa nane kuamkia leo (jana) katika hospitali ya General (Mkoa) Dodoma,” alisema Ndugai.

Ndugai alisema Tahir aliugua moyo kwa muda mfupi juzi usiku baada ya kutoka katika shughuli za Bunge salama na alikwenda hospitali mwenyewe kutibiwa na kuongeza akiwa katika matibabu alifariki.

“Tulikuwa naye huku ndani na tulifanya naye kazi vizuri. Alikuwa mmoja wa wabunge walioomba kwenda Urambo kumzika Spika mstaafu Sitta na alikuwa katika orodha ya wabunge,” alisema Ndugai kwa sauti ya majonzi huku Bunge likiwa na utulivu mkubwa.

Ndugai alimueleza Tahir kuwa alikuwa mcheshi, mwanamichezo mahiri, mbunge aliyejali sana wapiga kura wake, alijali wabunge wenzake bila kuangalia tofauti za kiitikadi.

Kutokana na kifo hicho, Spika Ndugai alimuomba Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu, Jenista Mhagama, kutengua Kanuni ya Bunge ya 152 inayohusu utaratibu Mbunge anapofariki.

Kanuni hiyo ya 152 inasema, “Endapo Mbunge atafariki wakati Bunge likiwa katika shughuli zake, Spika ataahirisha shughuli za Bunge kwa siku hiyo kwa ajili ya maombolezo.” Mhagama alitengua kanuni hiyo ili kuruhusu baadhi ya shughuli za Bunge kumalizika, ikiwemo majumuisho ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo pamoja na Kikao Maalum cha heshima za mwisho kwa mwili wa Sitta, kilichofanyika ndani ya Bunge jana.

Ndugai alisema kutokana na misiba hiyo miwili, baadhi ya wabunge watakwenda Zanzibar na wengine Urambo leo. Tahir alizikwa jana Unguja, Zanzibar kabla ya swala ya saa saba mchana.

Spika alisema wakati akitangaza mgawanyo huo, alisema, “siku ya leo imekuwa nzito sana, katika historia ya Bunge haijawahi kutokea. Wabunge tutamsindikiza mwenzetu hadi Uwanja wa Ndege Dodoma kuelekea Zanzibar.”

Wabunge walia nje ya Viwanja vya Bunge Nje ya Ukumbi wa Bunge, baadhi ya wabunge walishindwa kujizuia na kujikuta wakilia kutokana na kifo hicho.

Wabunge waliolia na wengine kusaidiwa kutulizwa na wenzao ni Mbunge wa Kiembe Samaki, Hassanali Mohamedali Ibrahim (CCM), Mbunge wa Same Mashariki na Mwenyekitiwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Naghenjwa Kaboyoka(Chadema) ambaye Tahir alikuwa mjumbe wa Kamati hiyo na Mbunge wa Viti Maalumu, Sophia Mwakagenda (Chadema).

Kutokana na kifo cha Tahir na cha Spika mstaafu Sitta, wakati wa salamu za rambirambi nje ya lango kuu la kuingia bungeni, Spika alitangaza kuwa posho za siku hiyo za wabunge zitagawanywa nusu itapewa familia ya Tahir na nyingine atapewa mjane wa Sitta, ambaye ni Mbunge wa Urambo, Margareth Sitta (CCM).

Mwili wa Tahir uliwasili nje ya lango kuu la kuingia bungeni saa 3:40 asubuhi na utaratibu wa kutoa heshima za mwisho kwa sheria za dini ya kiislamu na Bunge, ulifanyika.

Wabunge wazungumza

Wakitoa salamu za rambirambi, wabunge walimwelezea kuwa ni mtu aliyependa wenzake, mcheshi na aliyependa kazi yake pamoja na michezo. Akizungumza kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mbunge wa Kilolo, Venance Mwamoto alisema chama kinatoa ubani wa shilingi milioni tatu.

Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe (Chadema), alisema kifo cha mbunge huyo ni pigo lakini ni somo kwa wote kuwa maisha yapo mikononi mwa Mungu na kuongeza kuwa walikuwa pamoja katika uchaguzi wa wabunge mashabiki wa Yanga.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Serikali, aliwapa pole familia, mke na watoto wa marehemu na Bunge kwa kifo hicho.

“Ni kifo cha ghafla, hatukutarajia, tulikuwa naye pamoja jana (juzi), ameshiriki mambo ya kamati na wajumbe wenzake, tumekuwa naye kwenye michezo. Serikali kupitia Rais (John Magufuli) anakupa wewe Spika pole nyingi kwa msiba huu,” alisema Majaliwa.

Aliwakumbusha wabunge kuwa kila binadamu yupo safarini na kila mmoja ajenge uvumilivu na uhusiano mzuri na mwingine na kuiga mfano wa Tahir aliyekuwa akipenda majukumu yake na kuwapenda wengine.

Mbunge wa Tabora, Almasi Maige (CCM), alisema amefanya kazi na Tahir katika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge na kuongeza kuwa, wabunge watamkumbuka sana.

Wawakilishi katika msiba

Mbunge wa Ilala, Mussa Azzan Zungu alimwakilisha Spika katika maziko hayo huku Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi akiiwakilisha serikali. Dk Mwinyi pia ni Mbunge wa Kwahani, Zanzibar.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai baada ya kifo cha Mbunge wa Jimbo la Dimani Zanzibar, Hafidh Ali Tahir kilichotokea majira ya saa nane alfajiri kuamkia jana katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma.

Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu kwa vyombo vya harari ilimnukuu Rais akisema, “nimeshtushwa sana na kifo cha Hafidh Ali Tahir na ninakuomba Spika Job Ndugai unifikishie salamu za pole kwa familia ya marehemu, wabunge, wananchi wa Jimbo la Dimani, ndugu, jamaa na marafiki wote walioguswa na msiba huu. “Tutamkumbuka Tahir kwa mchango wake mkubwa alioutoa katika utumishi wa umma, katika michezo na akiwa mwakilishi wa wananchi, kwa hakika tumepoteza mtu muhimu sana.”

Swali alilouliza Tahir Bungeni Novemba Mosi, 2016 Tahir katika swali lake lililokuwa na vipengele viwili, alitaka kujua serikali haioni umuhimu wa kuweka utaratibu pindi mshindi akifa, aliyefuata kwa kura katika chama chake achukue nafasi hiyo.

Katika kipengele cha pili, Tahir alihoji Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka kuondoa utaratibu wa kusimamisha Uchaguzi Mkuu mgombea anapofariki.

Swali hilo lilijibiwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Walemavu, Dk Abdallah Possi ambaye alisema sheria za uchaguzi pamoja na mfumo wa uchaguzi uliopo nao unamwelekeza mpigakura kumpigia mtu (mgombea) na si chama kama ilivyo kwenye mifumo mingine ya kupiga kura ndani ya chama.

Alisema hivyo kwa sasa, Serikali itaendelea kutumia utaratibu uliopo kwa sababu mshindi wa pili atakayechukuliwa kujaza nafasi wazi, atakuwa hajachaguliwa na wananchi wote au jimbo au kata husika, bali wanachama wachache wa chama hicho.

Akijibu kipengele cha pili, Dk Possi alisema sheria ya sasa ya uchaguzi, Sura ya 343 inaelekeza kusimamisha Uchaguzi Mkuu nchi nzima anapofariki mgombea Urais au Makamu wa Rais na kufafanua kuwa kuwa, anapofariki mgombea ubunge au udiwani, uchaguzi mkuu huendelea nchi nzima isipokuwa katika jimbo au kata husika.

Wasifu wa marehemu

Tahir alizaliwa Oktoba 30, 1953, Dimani Mjini Magharibi Unguja. Alisoma elimu ya msingi katika Shule ya Kombeni Unguja mwaka 1957-1966. Mwaka 1985-1986 alisoma masuala ya habari na utangazaji radio huko Yugoslavia na baadaye aliendelea na masomo hayo Cairo, nchini Misri mwaka 1988-1990.

Kazi: Tahir alifanya kazi kama Mkufunzi wa Jeshi la Magereza Zanzibar mwaka 1970-1972. Mwaka 1972-1978 alikuwa Mkuu wa Kitengo cha Utangazaji Radio Zanzibar.

Siasa: Mwaka 1995 alikuwa Mnadhimu wa CCM Zanzibar, na mwaka 2003 aliteuliwa kuwa Katibu wa CCM Zanzibar, kazi aliyoifanya hadi mwaka 2005 alipochaguliwa kuwa Mbunge wa Dimani kwa tiketi ya CCM kwa vipindi vyote hadi alipofariki.

Amekuwa mjumbe wa Kamati ya PAC ya Fedha na Uchumi, ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge. Ameacha mjane, watoto saba.

ZeroDegree.
Vifo vyatikisa Bunge. Vifo vyatikisa Bunge. Reviewed by Zero Degree on 11/12/2016 11:46:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.