Loading...

CUF kujitoa UKAWA, ..2020 Kusimamisha mgombea wa kiti cha Urais

Baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba kusimamisha wagombea udiwani kwenye Kata 14 kati ya 20 katika uchaguzi mdogo wa marudio wa Januari 22,2017 Tanzania Bara na Baraza Kuu la Uongozi Taifa kukataa kusimamisha wagombea na kukiachia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kusimamisha katika kata zote kwa madai ya chama chake kuwa na mgogoro wa viongozi.

Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mahusiano ya Umma CUF anayetambuliwa na Lipumba, amesema kuwa kwa sasa shughuli zao zimejikita kukijenga chama hicho na si UKAWA kwa kuwa dhamira ya chama hicho ni kushika dola mwaka 2020.

Kambaya ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam, wakati akitoa tathmini ya uchaguzi mdogo wa madiwani uliofanyika mwezi huu, ambapo ametaja sababu ya vyama vya upinzani kushindwa katika uchaguzi huo, ni vyama hivyo kuishiwa nguvu pamoja na kushindwa kutetea ajenda ya ufisadi kwa madai kuwa vinakumbatia mafisadi.

Kambaya hakuishia hapo, amesema kuwa kwa sasa kila chama kinawajibu wa kujijenga huku akidai kuwa matokeo mazuri katika uchaguzi Mkuu wa 2015 ya vyama vinavyounda UKAWA hayakutokana na nguvu wala ushawishi wa umoja huo kupitia Edward Lowassa aliyekuwa Mgombea wa Chadema kwa mwamvuli wa umoja huo, bali yalitokana na nguvu za vyama hivyo.

“Kila chama kinahitaji kijijenge, uchaguzi uliopita hatukushinda sababu ya Lowassa. Uchaguzi huu umedhihirisha hilo sababu alipita katika kata zote lakini hawakushinda. 2015 tulishinda uchaguzi sababu ya nguvu za vyama vyetu,” amesema na kuongeza.

“2020 huenda kusiwepo UKAWA sababu ulilenga kutetea katiba itakua ajabu kutumia umoja huo ambao lengo lake ni tofauti, labda utafutwe umoja mwingine na jina lingine.”

Aidha, Kambaya amemtuhumu Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sheriff Hamad na wenzake kuwa wanatumia rasilimali za chama hicho kuijenga Chadema kwa mgongo wa UKAWA.

“Sasa kuna CUF inayofanya kazi Bara na inayofanya kazi Zanzibar, Katibu Mkuu na kundi lake lengo lao ni kuiua CUF Bara na ndiyo maana baadhi ya wabunge na viongozi wa CUF walisimama katika majukwaa kuwanadi wagombea wa Chadema ilhali katika maeneo husika kulikuwa na wagombea wa CUF,” amesema.

Ameongeza kuwa “Tatizo kwetu sio UKAWA, tatizo kwetu ni CUF, Ukawa utafuata baadae. UKAWA ni maridhiano baada ya kukijenga chama chetu.”

Source: DewjiBlog
CUF kujitoa UKAWA, ..2020 Kusimamisha mgombea wa kiti cha Urais CUF kujitoa UKAWA, ..2020 Kusimamisha mgombea wa kiti cha Urais Reviewed by Zero Degree on 1/30/2017 06:03:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.