Loading...

Simba, Yanga marufuku Taifa

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amesema kifungo cha Simba na Yanga kutotumia Uwanja wa Taifa kipo pale pale.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Nape alisema hawataruhusu mechi ya Simba na Yanga Februari 25 mwaka huu kuchezwa kwenye Uwanja wa Taifa, kwani ulishafungwa kutokana na kuharibiwa miundombinu.

Simba na Yanga zilikuwa zikitumia Uwanja wa Taifa kwa mechi zake za Ligi Kuu na zile za kimataifa, lakini baada ya Oktoba mosi mwaka jana Serikali ilitangaza kuzifungia kutumia uwanja huo kutokana na vurugu zilizosababishwa na mashabiki wa timu hizo ambao waling’oa viti na kuvunja mageti mawili.

“Hatutaruhusu mechi ya Simba na Yanga ichezwe taifa, kama wanasema wana mpango huo wanajifurahisha,” alisema.

Tangu kufungiwa kutumia uwanja huo, Simba na Yanga sasa zinacheza mechi zake za ligi kwenye uwanja wa Uhuru.

Awali, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) walihojiwa na waandishi wa habari kuhusu uwanja utakaotumika kwa mechi hiyo ambapo Ofisa Habari wake Alfred Lucas alisema watabeba jukumu la kuiomba Serikali iruhusu mechi ichezwe uwanja wa huo.

“Uwanja wa Uhuru hautakidhi mahitaji ya mashabiki wengi wa timu hizi, na kwa kutambua hilo tunatarajia kuchukua jukumu ya kuzungumza na serikali ili kuziombea timu hizi zicheze kwenye uwanja wa Taifa,” alisema.

Lucas alisema wako tayari kuingia makubaliano na serikali kuahidi kuulinda ilimradi Simba na Yanga zipewe uwanja huo mkubwa.

Alisema uwanja wa Uhuru ni mzuri lakini wanahofia mashabiki wengi watakosa nafasi kwani mchezo huo huingiza watu wengi uwanjani.

Tayari Yanga ilitangaza kuwa imepeleka ombi kwa serikali kuomba mechi zao za ligi zirudi Taifa lakini Waziri alisema hajapata barua hiyo.

Hii si mara ya kwanza kwa Yanga kuomba irudi kutumia uwanja huo, mwaka jana ilifanya hivyo ambapo serikali iliwaruhusu kuutumia kwa mechi za kimataifa pekee.

Source: Habari Leo
ZeroDegree.
Simba, Yanga marufuku Taifa Simba, Yanga marufuku Taifa Reviewed by Zero Degree on 1/25/2017 11:39:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.