Loading...

Huyu ndiye mwamuzi atakayechezesha mechi ya Simba na Yanga jumamosi

Mathew Akrama (katikati) atachezesha tena Simba na Yanga Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
REFA Mathew Akrama wa Mwanza ndiye atakayepuliza kipyenga katika mchezo wa watani wa jadi Simba na Yanga Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kikao cha Kamati ya Waamuzi kilichofanyika jioni ya leo mjini Dar es Salaam kimeteua Akrama kupuliza filimbi Jumamosi, wakati pembeni Mohammed Mkono wa Tanga na Hassan Zani wa Arusha watakimbia kimbia na vibendera.

Miamba hiyo ya soka ya nchini inatarajiwa kumenyana Jumamosi wiki hii Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa marudiano wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara. 

Simba na Yanga kwa sasa zipo kambini kujiandaa na mchezo huo wa Jumamosi, unaofuatia ule wa Oktoba 1, mwaka jana ambao zilitoka sare ya 1-1.
Yanga ambayo bao lake lilifungwa na Amissi Tambwe Oktoba 1, imeweka kambi Kigamboni, Dar es Salaam, wakati Simba iliyosawazisha kupitia kwa Shiza Kichuya imeweka kambi visiwani Zanzibar.

Hii ni mara ya pili kwa Akrama kuchezesha mechi ya watani, baada ya Oktoba 3, 2012 kuchezesha mechi ya Ligi Kuu pia timu hizo zikitoka sare ya 1-1 Uwanja wa Taifa. 

Katika mchezo huo ulioanza Saa 1:02 usiku, Akrama alimtoa kwa kadi nyekundu winga Simon Msuva wa Yanga dakika ya 77 kwa kumrudishia rafu beki wa Simba, Juma Nyosso.

Siku hiyo, Simba walitangulia kwa bao la kiungo Amri Kiemba dakika ya pili, kabla ya mshambuliaji Said Bahanuzi kuisawazishia Yanga dakika ya 63 baada ya beki Paul Ngalema kuunawa mpira kwenye boksi.

Lakini Akrama alilaumiwa kwa kumuonyesha kadi ya njano badala ya nyekundu kiungo wa Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ licha ya kumchezea rafu mbaya beki wa Yanga, Kevin Yondan hadi akashindwa kuendelea na mchezo, na nafasi yake ikachukuliwa na Juma Abdul.

Na pia alilaumiwa kuwa kutomchukulia hatua yoyote kipa Juma Kaseja aliyeonekana kupoteza muda tangu mwanzo, na alimpa onyo tu zaidi ya mara tatu.

Haikuwa ajabu Oktoba 6 Akrama alipoondolewa kwenye orodha ya wamuzi wa kuchezeaha Ligi Kuu baada ya kuvurunda mechi hiyo namba 80, huku aliyekuwa mshika kibendera namba mbili, Ephrony Ndissa wa Dar es Salaam akipewa onyo.
Huyu ndiye mwamuzi atakayechezesha mechi ya Simba na Yanga jumamosi Huyu ndiye mwamuzi atakayechezesha mechi ya Simba na Yanga jumamosi Reviewed by Zero Degree on 2/24/2017 11:03:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.