Loading...

Mbowe apewa masaa 48 ya kujisalimisha polisi

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, aliwafanyia 'umafia' na kuwaacha polisi wakimsubiri kwa siku tatu katika Kituo Kikuu cha Kanda Maalum ya Dar es salaam, na sasa jeshi hilo limempa saa 48 kuanzia jana ajisalimishe.

Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam inamtaka Mbowe sasa ajisalimishe Kituo Kikuu kesho ili ahojiwe kuhusiana na tuhuma zinazomkabili za dawa za kulevya.

Kamanda wa kanda hiyo, Kamishna wa Polisi, Simon Sirro, alimuamuru Mbowe kujisalimisha jana wakati akizungumza na waandishi wa habari na kueleza kuwa, kiongozi huyo alitoa taarifa kupitia baadhi ya viongozi (bila kuwataja) kuwa angefika Jumatano Kituo Kikuu cha Polisi lakini hakufanya hivyo.

Mbowe alitakiwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda kuripoti polisi kwa mahojiano baada ya kuwa mmoja wa watu 65 aliowataja kwamba wanahitaji kuchunguzwa kuhusu biashara ya mihadarati zaidi ya wiki moja iliyopita.

Lakini Mbowe ambaye ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Hai aliitisha mkutano na waandishi wa habari mjini Dodoma akipinga kutajwa hadharani, kutishia kumshitaki mahakamani mkuu wa mkoa huyo na kugomea wito.

Kumbe, hata hivyo, Mbowe aliahidi kufika polisi jijini Jumatano bila ya kutokea na jana alipewa saa 48 ajitokeze vinginevyo nguvu itatumika kumtafuta zaidi.

Kamanda Sirro alisema: “Kupitia baadhi ya viongozi walitujulisha kuwa Mbowe angekuja Jumatano kwa ajili ya kuhojiwa polisi dhidi ya tuhuma zinazomkabili za dawa za kulevya lakini jambo la ajabu hadi leo hajaja na mbaya zaidi jana (juzi) tumemtafuta kupitia simu yake ya mkononi hakupokea na baadaye aliizima.

“Tumemtafuta nyumbani kwake na mahali anakoishi sasa hivi, kote hayupo lakini maelezo yake bungeni amekuwa ni mpigaji vita mzuri wa dawa za kulevya, tunashangaa kwa nini amekataa kuitikia wito wetu kama yeye ni mmoja wa wale wanaopinga dawa za kulevya.”

Kamanda Sirro amemtaka kiongozi huyo asitafute namna nyingine ya kulikwepa jeshi la polisi.

“Sitegemei awe mtu wa kutafutwa, matumaini yetu baada ya ujumbe huu Jumatatu (kesho) ataitikia wito huu, sitegemei kuvutana naye, yeye ni kiongozi mkubwa na sheria ipo pale pale... hakuna aliyejuu ya sheria hata uwe kiongozi.”

WATU 65

Wiki iliyopita Makonda aliweka hadharani majina ya watu 65 wanaotakiwa kuchunguzwa kujihusisha na dawa za kulevya wakiwamo wanasiasa, wafanyabiashara wakubwa na wadogo na kiongozi mmoja wa dini.

Jina la Mbowe lilikuwa miongoni mwa wanasiasa waliotajwa ambao walitakiwa kujisalimisha polisi Ijumaa iliyopita kwa ajili ya mahojiano.

Mbowe alikanusha mbele ya vyombo vya habari kuhusika kwa njia yoyote ya kutumia, kufanya biashara hiyo wakati wote wa maisha yake.

Aidha, Mbowe alisema kuwa, chama chake kinakubaliana biashara hiyo ni hatari kwa ustawi wa taifa ambayo imeachiwa kushamiri kwa miaka mingi kwa sababu wahusika wakubwa ni washirika au ni wanachama wa Chama Cha Mapinduzi.

“Hatuungi mkono vita hii inavyopiganwa kwa hila na kinyume cha sheria,” alisema.

Aidha, alihoji kama Makonda ataweza kumlipa fidia kwa kumuhusisha na dawa za kulevya.

“Upumbavu huu siwezi kuukubali na Makonda atabeba mzigo huu, tutamfungulia mashtaka dhidi ya kashfa hii, sitaki uchunguzi wa polisi kuonyesha kuwa mimi ni mtu nisiye na hatia, najua mimi sina hatia.

“Sitaki polisi watangaze kuwa Mbowe hahusiki, hivi Makonda atanisafisha vipi kwenye hili? Ni kwa jiki au kwa kutumia nini? Mimi siwezi kwenda.

"Nipo tayari kuitwa na chombo chochote chenye mamlaka ya kisheria na sio Makonda.”

Vita mpya dhidi ya dawa za kulevya ilianza rasmi Februari 1 ambapo Makonda alitaja orodha ya awamu ya kwanza iliyohusisha wasanii na polisi 13.

Awamu ya pili ilihusisha majina 65, akiwamo Mbowe na katika awamu yake ya tatu, Makonda alikabidhi majina 97 kwa Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rogers Sianga Jumatatu.

Source: Nipashe
Mbowe apewa masaa 48 ya kujisalimisha polisi Mbowe apewa masaa 48 ya kujisalimisha polisi Reviewed by Zero Degree on 2/19/2017 02:04:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.