Loading...

Rais Magufuli amefuta agizo la Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe

Rais John Magufuli amelifuta agizo lililotolewa jana na Waziri wa Katiba na Sheria Harrison Mwakyembe linalotoa sharti la kuwa na cheti cha kuzaliwa kwa watu wote watakaofunga ndoa kuanzia Mei Mosi mwaka huu.

Rais Magufuli amefuta agizo hilo leo (Ijumaa) wakati akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi kabla ya kuondoka katika Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma na kurejea Jijini Dar es Salaam.

Amesema Serikali haiwezi kuruhusu sharti hilo kutumika kwa kuwa litawanyima haki ya kuoa na kuolewa Watanzania wengi ambao hawana vyeti vya kuzaliwa, huku utaratibu wa kupata vyeti hivyo ukiwa bado unakabiliwa na changamoto nyingi kwa wanaohitaji.


Amesema mpaka sasa idadi ya Watanzania walio na vyeti vya kuzaliwa ni chini ya asilimia 20 huku wengi wao wakiwa ni wananchi waishio vijijini ambako ni vigumu kupata vyeti hivyo, na wengine wakiwa ni waliozaliwa kabla ya kuanza kutolewa kwa vyeti vya kuzaliwa nchini mwaka 1961.

“Kwa hiyo ndugu zangu Watanzania msiwe na wasiwasi wowote, endeleeni na utaratibu wenu wa kuoa na kuolewa kama kawaida na kama kuna kifungu chochote cha sheria kinachomlazimisha mtu awe na cheti cha kuzaliwa ndipo aoe ama aolewe nitamuelekeza Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Harrison Mwakyembe apeleke Bungeni kikarekebishwe” amesema Rais Magufuli.

Hata hivyo Mhe. Rais Magufuli ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kupata vyeti vyao vya kuzaliwa kama kawaida na amewataka viongozi wote kuwahamasisha wananchi kuwa na vyeti hivyo.
Rais Magufuli amefuta agizo la Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe Rais Magufuli amefuta agizo la Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe Reviewed by Zero Degree on 3/17/2017 11:37:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.