Loading...

Serikali yapiga marufuku Semina za kujadili vifo vitokanavyo na uzazi

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu 
SERIKALI imepiga marufuku Semina zote za wadau kujadili vifo vitokanavyo na uzazi badala yake imeagiza fedha hizo zielekezwe kwenye ununuzi wa dawa na vifaa vya tiba kwa ajili ya akinamama wajawazito.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alitoa agizo hilo mjini hapa wakati wa hafla fupi ya kukabidhi vitanda 10 vya kujifungulia vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 8.5 alivyotoa Mbunge wa Viti Maalum, Aysharose Matembe ikiwa ni msaada kwa hospitali ya mkoa.

Mwalimu alisema kuwa semina za kujadili vifo vya uzazi zimekuwa zikigharimu fedha nyingi za umma wakati akina mama wajawazito pamoja na watoto wao wakipoteza maisha kutokana tu na uhaba wa madawa na vifaa tiba.

“Kuboresha Afya ya mama na mtoto sio suala la serikali peke yake bali ni jukumu la wadau wote wa sekta ya Afya.... Semina zimetosha. Kuanzia sasa, Semina hizo hazitaruhusiwa. Wasiendelee kuchezea fedha kwenye semina bali waboreshe huduma za Afya ya mama na mtoto” alisema na kuongeza, Kama kweli wanaguswa na tatizo hili kiasi hicho, basi wanunue vifaa tiba vya kutosha kwa ajili ya wajawazito kujifungulia ili kuokoa maisha ya vichanga hawa” alisema Waziri.

Hata hivyo, alieleza kuwa semina kwa ajili ya Mafunzo ya watumishi wa Afya zinazolenga kuboresha huduma kwa wajawazito na watoto zinaweza kuendelea kwa idhini yake au Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachewene.

Aidha, Waziri huyo ameahidi kuipatia hospitali hiyo gari kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa (ambulance) ili kupunguza makali ya baadhi ya changamoto zinazoikabili hospitali hiyo.

Akizungumza na wafanyakazi wa Sekretarieti ya mkoa pamoja na watumishi wa Afya, Waziri amehimiza uongozi wa Mkoa kuhakikisha unaweka mazingira mazuri kwa ajili ya watumishi wa Afya wanaopangiwa kwenda kufanya kazi mkoani humo ili wasitoroke kwenda maeneo mengine au kuacha kazi.
Serikali yapiga marufuku Semina za kujadili vifo vitokanavyo na uzazi Serikali yapiga marufuku Semina za kujadili vifo vitokanavyo na uzazi Reviewed by Zero Degree on 3/12/2017 02:10:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.