Loading...

Vincent Bossou awapa ujumbe mzito Yanga

AMA kweli pesa sabuni ya roho. Baada ya beki Vicent Bossou kulipwa fedha zake, amesema amezaliwa upya na sasa ni kuifanyia kazi nzuri timu yake ya Yanga.

Bossou aliingia katika malumbano na timu yake ya Yanga baada ya kuibuka na kudai kuwa anaidai klabu hiyo malimbikizo ya mshahara wa miezi minne.

Akizungumza na waandishi wa habari, Bossou alisema hatua ya klabu hiyo kumlipa fedha zake imemfanya ajione ana nguvu mpya za kuweza kuitumikia na kuipa mafanikio.

Alisema siku zote amekuwa akiichezea Yanga kwa mapenzi makubwa, ambapo alichukua fursa hiyo kuwaomba radhi mashabiki wa timu hiyo kutokana na kukosekana kwake katika baadhi ya mechi.

“Nashukuru nimepata haki yangu, niseme kitu kimoja, kazi ndiyo imeanza, ni kama nimezaliwa upya, nawaomba mashabiki wanisamehe baada ya kuniona kama msaliti kipindi chote nilipokosekana uwanjani,” alisema Bossou.

Alisema kuelekea katika mchezo wao wa leo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Zanaco utakaopigwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, amejipanga kufanya makubwa na kuwapa furaha mashabiki wa timu hiyo.

“Ni mchezo muhimu kwetu, tutajitahidi kucheza kufa na kupona. Kwa upande wangu nimejipanga kuwadhibiti washambuliaji wa Zanaco kwa kuhakikisha hawaleti madhara kwetu,” aliongeza Bossou.

Beki huyo raia wa Togo alisema wanaupa uzito mkubwa mchezo wa leo, kwakuwa wanahitaji ushindi mnono ili wajiweke kwenye mazingira mazuri ya kushinda mchezo wa marudiano utakaofanyika nchini Zambia.

Yanga itashuka dimbani leo kuanzia saa 10 jioni kuivaa Zanaco katika pambano la raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika, litakalopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Source: Bingwa
Vincent Bossou awapa ujumbe mzito Yanga Vincent Bossou awapa ujumbe mzito Yanga Reviewed by Zero Degree on 3/11/2017 06:20:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.