Loading...

Polisi yaamuru wasafiri kudai tiketi kila wanaposafiri

Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Ruvuma, Abel Swai akikagua kitabu cha tiketi kinachotumiwa na moja ya daladala zinazofanya safari zake kati ya Stendi Kuu Songea kwenda Kijiji cha Mletele katika Manispaa ya Songea akiwa katika ukaguzi wa magari na madereva wanaokiuka sheria za usalama barabarani.
WASAFIRI na wakazi wa Mkoa wa Ruvuma wametakiwa kujenga tabia ya kudai tiketi kila wanaposafiri kwani kufanya hivyo itawasaidia na itakuwa rahisi kupata msaada pindi yanapotokea matatizo wakiwa safarini.

Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Ruvuma, Abel Swai amesema hayo mjini Songea wakati akifanya operesheni kabambe ya ukaguzi wa magari na madereva wanaovunja sheria za usalama barabarani ambao ni chanzo cha ajali zinazotokea.

Aidha, katika ukaguzi huo, magari mengi hasa daladala yanayofanya safari kati stendi kuu mjini Songea kwenda Hospitali ya Mtakatifu Joseph Peramiho, Mletele, Lilambo, Matogoro, Mtakanini, Liweta yalibainika kuwa na makosa mengi ikiwemo uchakavu na kukosa vifaa muhimu kama vya kuzimia moto.

Mbali na hivyo, madereva na kondakta kutokuwa na sare, kujaza kupita uwezo wa gari, kutowapa tiketi abiria na hata wale waliokutwa na sare, zilikuwa chafu na nyingine kutoa harufu kali jambo linalosababisha kero kwa abiria wao.

Swai alisema kwa muda mrefu kumekuwa na tabia ya baadhi ya madereva na makondakta wa daladala kutozingatia sheria zilizopo, jambo linalosababisha wananchi kushindwa kupata haki yao mara gari linapopata tatizo kwani baadhi ya madereva na makondakta wao hukimbia na kusababisha upotevu wa mali.

Alisema, suala la kutoa tiketi kwa abiria lipo kisheria na makondakta wanatakiwa kuhakikisha kwamba wamiliki wa magari wanawapa vitabu vyenye kuonesha jina la gari, mmiliki, anuani ya mmiliki pamoja na konda kuandika majina mawili ya abiria wake itakayoambatana na tarehe ya siku ya safari.

Source: Habari Leo
Polisi yaamuru wasafiri kudai tiketi kila wanaposafiri Polisi yaamuru wasafiri kudai tiketi kila wanaposafiri Reviewed by Zero Degree on 4/06/2017 01:21:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.