Loading...

Sakata la ombaomba wa jijini Dar latua Bungeni

SAKATA la ombaomba jijini Dar es Salaam, limetua bungeni huko ikielezwa kuwa, wanatishia hadhi ya jiji hilo kutokana na kulichafua kwa kiasi kikubwa. Hayo yalisemwa bungeni wiki iliyopita na Mbunge wa Kiembesamaki, Ibrahim Raza (CCM) aliyeitaka serikali kuchukua hatua za haraka kukabiliana na hali hiyo.

“Wakiachwa watapakae, hadhi ya Dar e Salaam hasa katikati ya jiji hilo iko hatarini kushuka. Pamekuwa na ombaomba ambao usiku wanaweka magodoro, wanaweka vyandarua na kulala, asubuhi wanaamka na kuoga.

Kwa kweli mandhari ya Jiji la Dar es Salaam inapotea kabisa,” alisema Raza.
 
Aliyasema hayo wakati akichangia hoja ya bajeti ya Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) iliyopo chini ya Ofisi ya Rais iliyokuwa inaombewa kiasi cha Sh trilioni 6.5, sawa na karibu asilimia 20 ya bajeti yote ya serikali katika mwaka ujao wa fedha za 2017/18.

Bajeti hiyo ilipitishwa usiku wa Alhamisi. Raza alisema inashangaza kuona mambo hayo yakifanyika katikati ya jiji ambako viongozi wake na Manispaa zake wametapakaa, lakini wanashindwa kushughulikia suala hilo.

“Haya ya uchafu hawayaoni, mitaa ya katikati ya jiji inanuka kwa uchafu, watu wanaoga na kujisaidia hovyo haja zao…lakini wafanyabiashara nyakati za usiku wanawaona na kuwabughudhi… inakera sana.

Naomba serikali isiache hali hii iendelee. Akizungumzia wafanyabiashara wakiwemo wa mishikaki, chipsi, nyamachoma na kadhalika katika mitaa ya jiji, alishangaa kuona wanabughudhiwa na hata kuvunjiwa biashara zao, pengine kwa sababu tu ya kushindwa kutoa rushwa, huku akishauri badala ya kujenga uadui na wafanyabiashara wanaojitafutia riziki, serikali ione umuhimu wa kuigeuza hiyo kuwa fursa ya kuongeza mapato, kwa kuanza kutoza ushuru maalumu.

“Mheshimiwa Magufuli anapiga vita rushwa, lakini baadhi ya hawa watu wa Manispaa wanaendekeza rushwa. Nashauri, uandaliwe utaratibu wa kuhalalisha shughuli zao ili walipe kodi. Kuna mitaa kule Bangkok (Thailand) ikifika saa 12 mpaka saa sita usiku wanaruhusiwa.

Hawa wenzetu wa Dar es Salaam ni tofauti, hili liangaliwe upya. Serikali yetu inafanya kazi nzuri lakini wachache wanaitia doa,”
alisema Raza.

Akijibu hoja hizo, Simbachawene alisema amepokea hoja hizo na kwa kuwa serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli ni sikivu, yote yatafanyiwa kazi.
Sakata la ombaomba wa jijini Dar latua Bungeni Sakata la ombaomba wa jijini Dar latua Bungeni Reviewed by Zero Degree on 4/24/2017 04:41:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.