Loading...

Dereva wa gari alivyokufa maji akijaribu kuokoa maisha ya bodaboda kwenye Mafuriko

  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Hassan Nassir Ali.
MTU mmoja mkazi wa Fuoni amefariki dunia akiwa katika juhudi za kumuokoa jamaa yake aliyekuwa amezidiwa na maji ya mafuriko.

Mkasa huo ulitokea kwenye dimbwi kubwa la maji ya mvua lililopo katika eneo la Kibonde Mzungu, eneo la Barabara ya Fuoni, Unguja.

Mohammed Abdallah (42) aliyekuwa dereva wa gari la abiria linalosafirisha abiria katika eneo la Tunguu, alikutwa na mauti hayo baada ya kujitosa majini kumuokoa Paulo Salum (41).

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Hassan Nassir Ali, alisema marehemu na Salum walikuwa wakifahamiana.

Kabla ya kukutwa na mauti, marehemu aliweka gari pembeni na kwenda kumuokoa mwenzake huyo ambaye alipita eneo hilo akiendesha pikipiki, lakini akasombwa na maji.


“Huyu marehemu alikuwa anamfahamu manusura, sasa baada ya kuona ameanguka na kusombwa na maji alijidhatiti na kuweka gari pembeni, na kujitosa katika maji hayo mengi yaliyotuwama ili kwenda kumuokoa,” alisema. 

Ali alisema tukio hilo la jana saa 3:30 asubuhi ni la pili mwezi huu katika eneo hilo baada ya askari polisi kufariki dunia kwa kusombwa na maji pia mapema.
Alisema vikosi vya uokoaji vilifika katika eneo kumuokoa Salum na kuopoa mwili wa marehemu Abdallah.

Alisema manusura alikimbizwa hospitalini.

“Taratibu za kuukabidhi mwili wa marehemu kwa familia yake kwa ajili ya mazishi zinaendelea kufanyika.” 

Aidha, Kamanda Ali alisema ni marufuku kwa vyombo vya usafiri vidogovidogo kupita katika barabara hiyo na eneo hilo la Kibonde Mzungu ambalo limetuwama maji.

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohammed Mahmoud, alisema kifo hicho kimesababishwa na uzembe wa manusura kwa sababu alipewa tahadhari na askari wa usalama wa barabarani kuwa asipite njia hiyo, lakini akakaidi agizo hilo.

Alisema serikali ina mpango wa kuweka kizuizi katika eneo hilo la barabara ili kuzuia ajali zaidi.
Dereva wa gari alivyokufa maji akijaribu kuokoa maisha ya bodaboda kwenye Mafuriko Dereva wa gari alivyokufa maji akijaribu kuokoa maisha ya bodaboda kwenye Mafuriko Reviewed by Zero Degree on 5/23/2017 11:19:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.