Loading...

Kijana aliyeua bibi yake kwa mpini wa jembe amehukumiwa kwenda jela miaka 20


MKAZI wa Mji mdogo wa Sirari wilayani Tarime mkoani Mara, Musa Said(24) amehukumiwa kwenda jela miaka 20 baada ya kupatikana na hatia ya kumuua bibi yake, Veronika Amos kwa kumpiga kwa mpini wa jembe na jiwe kichwani.

Alisomewa hukumu hiyo katika kesi namba 65/2013 Mei 26 mwaka huu na Jaji Rose Ebrahim wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza katika kikao cha mahakama hiyo kinachoendelea Mahakama ya Wilaya ya Tarime.

Upande wa mashitaka ukiongozwa na Mwanasheria wa Serikali, Venance Mayenga ulidai kuwa mtuhumiwa huyo, Said, alitenda kosa hilo Desemba 23 mwaka 2011 wakiwa nyumbani kwao, ambapo alimshambulia bibi yake kwa kumpiga kwa mpini wa jembe na jiwe kichwani na kumsababishia majeraha, hali iliyosababisha kifo chake.

Upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili wa Kujitegemea, Baraka Makowe ulidai kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo akili zake zikiwa haziko sawa na kwamba mtu huyo alikuwa amelewa pombe na kuvuta bangi.

Hoja hizo za utetezi, zilipingwa na wakili wa serikali aliyedai kuwa mtuhumiwa akijua kuwa aliyemshambulia na kumsababisha kifo chake, alikuwa bibi yake, aliyekuwa anategemewa na familia hiyo.

Alisema unywaji wa pombe wa mtu mwenyewe hauwezi kuwa kinga ya kusamehewa kosa na kwamba hakuna vielelezo vyovyote, vinavyoonesha kuwa mtuhumiwa alikuwa amelewa.

Hivyo, alisema kitendo alichokifanya ni cha ukatili kwa bibi yake na hakiwezi kuungwa mkono na jamii. Jaji Rose Ebrahim aliungana na upande wa mashitaka na kusema mtuhumiwa alikiri kufanya mauaji hayo ya bibi yake, Veronika.

Pia, Jaji alisema mbali na mtu huyo kudai kuwa alikuwa amelewa, pombe alikunywa mwenyewe bila kunyweshwa na mtu mwingine, hivyo inadhihirisha kuwepo nia mbaya ya kufanya kosa.

Kwa hali hiyo, Jaji huyo alisema anaungana na wazee wa mahakama na wakili wa Serikali na kumhukumu mtu huyo kwenda jela miaka 20 ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye nia kama hiyo.
Kijana aliyeua bibi yake kwa mpini wa jembe amehukumiwa kwenda jela miaka 20 Kijana aliyeua bibi yake kwa mpini wa jembe amehukumiwa kwenda jela miaka 20 Reviewed by Zero Degree on 5/28/2017 06:32:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.