Loading...

Polisi watumia mabomu kuwatawanya madiwani kwenye Mgodi wa Dhahabu Geita


Polisi wametumia mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi na madiwani waliofunga barabara ya kuingia kwenye Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM).

Katika tukio hilo leo Alhamisi asubuhi, madiwani wawili na baadhi ya wananchi wamekamatwa na polisi.

Kabla ya kutumia mabomu, polisi walitoa onyo wakiwataka wananchi na madiwani hao kutawanyika kwa amani lakini waligoma.

Madiwani wa halmashauri mbili za Wilaya ya Geita jana Jumatano walitangaza mgogoro na GGM wakishinikiza kulipwa Dola milioni 12 za Marekani zinazotokana na ushuru wa huduma kuanzia mwaka 2004 hadi 2013.

Walitangaza kuzuia magari ya mgodi kwa kufunga barabarana pia kufunga maji yanayoingia mgodini kutoka Ziwa Victoria.

GGM iliwatangazia wafanyakazi wake jana kutofika kazini leo kutokana na mgogoro huo.

Polisi hivi sasa wameimarisha ulinzi kwenye maeneo ya Nungwe uliko mradi wa kusambaza maji mgodini, eneo la uwanja wa ndege na geti la kuingia mgodini.

Mkuu wa Wilaya ya Geita, Herman Kapufi na mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Musukuma wameingia mgodini baada ya madiwani na wananchi kutawanywa.
Source: Mwananchi
Polisi watumia mabomu kuwatawanya madiwani kwenye Mgodi wa Dhahabu Geita Polisi watumia mabomu kuwatawanya madiwani kwenye Mgodi wa Dhahabu Geita Reviewed by Zero Degree on 9/14/2017 08:06:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.