Loading...

“Mila ya ukeketaji ni mbaya, ina madhara makubwa ya kiafya" - Anna Mghwira


Mwenyekiti wa bodi ya shirika lisilo la kiserikali la Empower Society Transform Lives (ESTL), Anna Mghwira, ameshauri kupigwa marufuku faini zote za kimila zilizopitwa na wakati, ikiwemo faini ya ‘njughuda, kwa madai zinachangia kuendelezwa kwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na ukeketaji.

Amesema faini hizo za kimila, hazina makali hivyo haziwezi kuongofya watu kuendelea kujihusisha na vitendo hivyo vilivyo kinyume na haki za binadamu.

Amefafanua, kwa kusema faini hizo zinatolewa na pande mbili ambazo ni upande wa wanyanyasaji, na ule wa mwaathirika.

Akifafanua zaidi, amesema pande hizo, huwa hazina uwezo wa kubaini madhara ya muda mfupi na mrefu kwa muathirika wa tendo la unyanyasaji wa kijinsia. Kipaumbele cha upande wa mwaathirika, ni kupata fidia yo yote ,hata iwe ni ndogo kiasi ngani.

Mwenyekiti huyo ambaye ni mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, ametoa ushauri wake huo juzi, kwenye hafla ya uzinduzi wa mradi wa kutokomeza ukeketaji mkoani Singida (Kick FGM out of Singida).

Mghuwira lisema ili lengo la mradi huo awamu ya pili yaweze kufikiwa, ni mila zilizopitwa na wakati za kupeana adhabu ya kulipa fidia za kimila, ipigwe vita kwa nguvu zote.

Mwenyekiti huyo,alisema mradi huo unatekelezwa kwa ufadhili wa shirika la The Foundation for Civil Societyna uhai wake ni miaka miwili.

“Tunatoa wito kwa wakazi wa mkoa wa Singida, sote tuimbe na wimbo wetu moja nao ni kutokomeza ukatili wa kinjisia na ukeketaji kwa wanawake, na hasa watoto wa kike hasa katika jamii ya kabila la Wanyaturu,” alisema.

“Mila ya ukeketaji ni mbaya, ina madhara makubwa ya kiafya kwa watoto wa kike na wanawake wote, kwa ujumla. Hivyo basi tunalazimika kushirikiana sote na kutafuta rasilimali, ili tuitokomeze mila hii,” alisema.

Kwa upande wake mgeni rasmi katika uzinduzi huo mkuu wa mkoa wa singida Dk. Rehema Nchimbi, amesema malengo ya mradi huo ya kufikia kata 15 hadi kufikia ukomo wa uhai wa mradi, yanampa imani kwamba vitendo vya ukatili wa wanawake katika mkoa wa Singida, vitatokomezwa.

“Fanyeni bidii, imarisheni kazi yenu, shirikianeni na wadau wengine wa maendeleo. Na sisi katika serikali ya mkoa tutawaunga mkono na kuwapa ushirikiano viongozi kutoka maeneo ya mradi ulipo. Ninaamini watashirikiana na ESTL, kuhakikisha mradi huu wa kutokomeza vitendo hivi vya ukatili wa kijinsia hususani, ukeketaji, unafanikiwa malengo yake,” alisema.

Akisisitiza, amesema amesikitishwa na mbinu mpya ambayo imeshamiri ya ukeketaji wa watoto wachanga mara tu wanapozaliwa.

“Hili ni jambo la hatari sana kwa watoto wetu na ni lazima kila mmoja wetu ashiriki kwa nafasi yake kutokomeza vitendo hivi. Ukatili ni kitendo kibaya kinachokiuka haki ya mwanamke, kinadhalilisha utu wa mwanamke na kinakiuka haki za binadamu,” amesisitiza zaidi.
“Mila ya ukeketaji ni mbaya, ina madhara makubwa ya kiafya" - Anna Mghwira “Mila ya ukeketaji ni mbaya, ina madhara makubwa ya kiafya" - Anna Mghwira Reviewed by Zero Degree on 1/07/2018 10:50:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.